Wewe ni kijana? Unakidhi vigezo vya JKT? kama ndiyo, JKT wanakuhitaji kuanzia sasa

JESHI la Kujenga Taifa (JKT) limetangaza nafasi  za kujiunga na mafunzo ya jeshi hilo kwa kujitolea kwa mwaka 2020, anaripoti Frank Mvungi kutoka MAELEZO.

Mkuu wa Tawi la Utawala wa Jeshi hilo, Kanali Julius Kadawi  ameyabainisha hayo jijini Dodoma katika makao makuu ya jeshi hilo yaliyopo mjini Chamwino jijini Dodoma.

Amesema kuwa, Mkuu wa Jeshi hilo Meja Jenerali Charles Mbuge anawatangazia vijana wote wa Tanzania Bara na Visiwani nafasi za kujiunga na mafunzo hayo ili waweze kujengewa stadi za kuweza kujiajiri na kuwa wazalendo.

“Jeshi la Kujenga Taifa linapenda kuwaarifu vijana watakaopata fursa hiyo kuwa halitoi ajira kwa vijana, pia halihusiki kuwatafutia vijana ajira katika asasi, vyombo vya ulinzi na usalama na mashirika mbalimbali ya Serikali na yasiyo ya Kiserikali,"amesisitiza Kanali Kadawi.

Ameongeza kuwa, uratibu wa vijana kuomba na hatimaye kuchaguliwa kujiunga na mafunzo hayo, unaratibiwa na ofisi za wakuu wa mikoa na wilaya ambako mwombaji anaishi.

Akifafanua amesema kuwa, jeshi hilo linatoa mafunzo ambayo yatawasaidia vijana kujiajiri wenyewe mara baada ya kumaliza mkataba wao na JKT.
Mkuu wa  Tawi  la Utawala Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Kanali  Julius Kadawi akisisitiza kuhusu nafasi zilizotolewa kwa vijana wanaopenda kujiunga na Jeshi hilo kwa kujitolea kwa mwaka 2020, hayo yelijiri Agosti 20, 2020 Makao Makuu ya jeshi hilo Chamwino mkoani Dodoma. 
(Picha na MAELEZO/Diramakini).


“Kutokana na ugonjwa wa homa kali ya mapafu (COVID- 19), tahadhari za kuzuia maambukizi ya ugonjwa huo kama zilivyoelekezwa na Serikali kupitia Wizara ya Afya zitazingatiwa kwa kipindi chote vijana watakapokuwa katika mafunzo,”amesisitiza Kanali Kadawi.

Aidha, amebainisha  kuwa Meja Jenerali Charles Mbuge anawaalika vijana wote watakaopata fursa hiyo kwenda kujifunza uzalendo, ukakamavu, stadi za kazi, stadi za maisha na pia kuwa  tayari kulilinda na kulitumikia Taifa.

Baadhi ya sifa za vijana wanaotakiwa ni pamoja na; kuwa raia wa Tanzania, awe na afya njema, mwenye nidhamu na tabia nzuri na hajawahi kupatikana na hatia Mahakamani na hajawahi kufungwa, asiwe ametumikia Jeshi la Magereza, Polisi, KMKM, Chuo cha Mafunzo, wala kuajiriwa na idara nyingine serikalini.

Kigezo kingine asiwe amepitia JKT katika operesheni za nyuma, asiwe amejihusisha na matumizi ya dawa za kulevya. 
 
Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limekuwa likiwaandaa vijana kujiajiri kwa kuwajengea stadi za maisha na kuwawezesha kuwa wazalendo, waadilifu na walio tayari kulilinda Taifa.

Karibu! Tovuti hii ya www.diramakini.co.tz imesajiliwa rasmi na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na kupewa leseni namba TCRA/OCS-BL/0197/2020 chini ya Diramakini Business Limited iliyosajiliwa nchini Tanzania kwa ajili ya kukuhabarisha, kukuelimisha na kukupasha habari mbalimbali toka ndani na nje ya nchi. Je? Una habari,maulizo au tangazo, unataka kutupa ufadhili? Tuwasiliane; diramakini@gmail.com Asante.

 

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news