DED Moshi: Shilingi Bilioni 60 zimetumika katika miradi ya maendeleo, Stendi ya Kimataifa Moshi kuweka rekodi Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati

Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro, Michael Mwandezi amesema zaidi ya shilingi Bilioni 60 zimetumika katika miradi ya maendeleo kwa kipindi cha miaka mitano katika Manispaa ya Moshi ikiwemo kuweka taa za barabarani mjini Moshi, anaripoti Pius Ntiga, Moshi.

Kiasi hicho cha fedha ni kuanzia mwaka 2015-2020 katika Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli, ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2015-2020.Katika mahojiano na Amsha Amsha 2020 ya Uhuru FM, leo Mkurugenzi huyo wa Manispaa ya Moshi, ameipongeza Serikali kutokana na kupelekwa kwa kiasi hicho cha fedha.

Chini ya fedha hizo zaidi ya shilingi Bilioni 2 zimetumika katika ujenzi wa Stendi Kuu ya Kimataifa ya Mabasi ya mikoani iliyopo eneo la Ngangamfumuni nje kidogo ya Mji wa Moshi.
Ujenzi wa stendi hiyo uliopo chini ya Kampuni ya CRJE (East Africa) ulianza mwaka 2019 na unatarajiwa kukamilika mwaka 2021.

Aidha, Mkurugenzi huyo wa Manispaa ya Moshi amesema, stendi hiyo itakuwa na uwezo wa kuegesha magari madogo 300 na kwamba itakuwa na uwezo kuchukua mabasi 70 kwa wakati mmoja.

Pia ujenzi huo amesema umechochea ajira zaidi ya elfu kumi ambapo kazi ya hizo zipo ajira ya muda mfupi na mrefu ambazo ni mia nne.

 "Niwaambieni tu kuwa mradi huu wa Stendi ya Moshi utakuwa mkubwa nchini na utauzidi pia ule wa Mbezi Mwisho jijini Dar es salaam,"amesema Mkurugenzi. Pia kilomita 16 za barabara amesema zina lami na taa za barabarani Mjini Moshi.

Aidha, miradi huo wa Stendi Kuu ya mabasi jengo lake litakuwa na ghorofa mbili na kutakuwa na hoteli na maduka makubwa na kwamba mkandarasi wa ujenzi huo ndiye aliyejenga Daraja la Kigamboni jijini Dar es salaam.Amesema, jengo la stendi hiyo kuu litakuwa pia na ofisi za Kimataifa za Uhamiaji.

Miradi mingine iliyotekeleza katika Manispaa ya Moshi ni pamoja na Mradi wa Dampo la kisasa la Mtakuja lililopo kilomita 15 kutoka Moshi Mjini hadi eneo la Mtakuja.

Mradi huo ulianza kujengwa mwezi Juni mwaka 2019 na tayari limeshaanza kufanya kazi na litahudumia wakazi wote wa Manispaa ya Moshi.

Akizungumza na Amsha Amsha 2020 ya Uhuru FM, Mhandisi wa Manispaa hiyo, Richard Sanga amesema,mradi huo unatekelezwa na kampuni ya Rocktonic na kwamba zaidi ya shilingi bilioni mbili zimetumika katika ujenzi wake.

Mhandishi Sanga amesema eneo la mradi huo lina ukumbwa wa hekari 15 na ndani ya mradi huo kutajengwa Kiwanda cha mbolea kinachotokana na takataka zinazotupwa katika dampo hilo.

"Tayari mashine kwa ajili ya Kiwanda cha Mbolea zimeshanunuliwa na zinasubiriwa kufungwa na wananchi watanufaika na mbolea inayotokana na mabaki ya chakula,"amesema

"Wananchi waliopo jirani watanufaika na Dampo hilo,hivyo waanze kuleta taka zao hapa na takataka zitakazotupwa hapo ni zile zisizooza,"amesema.

Aidha, Mhandisi Sanga amesema tayari elimu kwa wananchi wameshaanza kupewa kuhusu namna na kutunza taka zinazooza kwa manufaa ya kuzipeleka ili zikatengenezwe mbolea.

Pia amesema, dampo hilo la kisasa limetengezezwa kisasa hata mvua ikinyesha halitajaa kwani kuna chemba za kupitisha maji zimejengwa chini li kuruhusu maji kutoka nje.

Katika kulinda mazingira chini ya dampo hilo umewekwa nailoni ili kutoharibu mazingira chini yake zimewekwa.

Aidha, dampo hilo baada ya miaka minane amesema litajaa na kuwa mwisho wa matumizi na badala yake litabadilishwa matumizi na kuwa sehemu ya bustani.

Katika hatua nyingine Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli imepeleka katika Shule ya Sekondari ya Ufundi Moshi, Shilingi Bilioni Mbili kwa ajili ya ukarabati wa shule hiyo kongwe inayofundisha pia masuala ya ufundi kwa wanafunzi wa kidato cha nne na cha sita.

 Mkuu wa shule hiyo, Erasmus Kyara amesema shule hiyo ipo katika Kata ya Karanga na ni miongoni mwa shule kongwe zilizokarabatiwa na Serikali.
"Shule hii ilianzishwa mwaka 1957 na mimi mwalimu Kyara ni mwalimu wa kumi na saba kuwa mkuu wa shule hii tangu kuanza kwake,"amesema Kyara.

Amesema, ukarabati katika shule hiyo umehusisha jengo la utawala, mabweni 40 ya wavulana na bweni moja la wasichana, madarasa matatu, maabara pamoja na jengo la maktaba yenye uwezo wa kuchukua watu 200 na ukarabati wa majiko.

Aidha amesema ukarabati huo umehusisha mfumo wa Tehama na ukarabati wa karakana na ukarabati wa matundu ya vyoo.

Kwa mujibu wa Kyara ukarabati huo umefanya walimu kufanya kazi zao vizuri na wanafunzi kusoma vizuri na ufaulu umeongezeka kwa zaidi ya asilimia 70.

Nao baadhi ya wanafunzi katika shule hiyo wameipongeza Serikali kwa kufanya ukarabati wa shule yao kongwe ambayo wamesema hali hiyo imesaidia ufaulu kuongezeka na walimu kuipenda kazi yao ya kufundisha.

Wamesema, mabweni yalikuwa hayana milango na madirisha, vyoo vilikuwa ni hatarishi kwa afya zao,lakini sasa hali ni nzuri sana, hivyo wanaishukuru serikali.

Pia wameomba idadi ya walimu iongezeke shuleni hapo kwani wana upungufu wa walimu 16, hivyo wakipewa itapunguza changamoto ya upungufu wa walimu wa ufundi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news