DKT.MABULA: SERIKALI INATAMBUA MCHANGO WA MADHEHEBU YA DINI NCHINI

SERIKALI ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt.John Magufuli inatambua mchango wa madhehebu mbalimbali ya dini nchini kwa kuisaidia kutoa huduma muhimu kwa jamii kama vile elimu na afya.

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi,Dkt.Angeline Mabula wakati wa kufunga sherehe za makambi kwa dhehebu la Kanisa la Waadventista Sabato zilizofanyika katika viwanja vya kanisa hilo Mtaa wa Nyakato jijini Mwanza.

Dkt.Mabula amelishukuru kanisa kwa kuunga mkono jitihada za Serikali kwa kutoa huduma kwa jamii kupitia taasisi zake kama vile elimu kwa shule inazozimiliki na huduma za afya zinazotolewa na hospitali zake pamoja na vituo vya afya huku akilipongeza kwa kuungana pamoja na madhebu mengine ya dini katika kuliombea taifa wakati wa janga la ugonjwa wa Covid-19.

"Serikali inatambua, inathamini na inashukuru kwa mchango wenu katika kuleta maendeleo ya nchi,"amesema Dkt.Mabula.

Dkt.Mabula amewataka waumini wa kanisa hilo kutumia kipindi hiki cha uchaguzi kwa kuliombea taifa kuwa na amani na utulivu sanjari na kuchagua viongozi wazuri na wenye hofu ya Mungu kama Rais Dkt.John Magufuli ili nchi iweze kupata maendeleo.Kwa habari nyingine soma hapa.

Kwa upande wake Mnenaji Mkuu wa kambi hilo, Mchungaji Sadikiel Shehemba amefafanua kuwa kambi la Sabato kwa mwaka wa 2020 lilianza Agosti 30, mwaka huu kabla kuhitimishwa kwake huku likipambwa na kauli mbiu ya 'Mungu Kwanza Mengine Baadae, Yesu anakuja tujiandae' sambamba na kusisitiza juu ya ubatizo na umuhimu wake kwa waumini wa kanisa hilo.

Akihitimisha mmoja wa waumini aliyehudhuria kambi hilo katika mahojiano na www.diramakini.co.tz  Marygoreth John mbali na kuishukuru Serikali kwa kutofungia wananchi wake katika kipindi cha janga la ugonjwa wa Covid-19 kama zilivyofanya baadhi ya nchi amempongeza Naibu Waziri Dkt.Mabula kwa namna anavyoshirikiana na jamii yake bila kujali tofauti za kidini, kabila au rangi.


Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news