Mgombea Ubunge Ilemela, Dkt.Angeline Mabula aahidi maendeleo

MGOMBEA Ubunge wa Jimbo la Ilemela jijini Mwanza kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt.Angeline Mabula amesema kuwa ataendelea kuwatumikia wananchi wa Jimbo la Ilemela kwa haki, usawa na uadilifu mkubwa kuhakikisha wananchi hao wanapata maendeleo.

Dkt.Angeline Mabula ameyasema hayo wakati akihutubia mamia ya wafuasi wa chama hicho na wananchi katika mkutano wa hadhara wa kampeni ya uchaguzi uliofanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi Masemele Kata ya Shibula.

Mgombea huyo amewataka wananchi hao kuchagua viongozi wanaoweza kuwatumikia na kuwaletea maendeleo badala ya kujaribu watu wasiokuwa na maono ya kutumikia watu zaidi ya kujinufaisha wao binafsi huku akibainisha miradi mbalimbali ya maendeleo iliyotekelezwa ndani ya jimbo hilo kwa kipindi cha miaka mitano ya utawala wake na wa Rais Dkt.John Magufuli.

Amesema katika kipindi hicho hospitali ya wilaya imejengwa, shule mpya tatu za msingi na sekondari zimejengwa, miradi mikubwa ya maji imejengwa na urasimishaji wa makazi na umilikishaji ukifanyika kikamilifu huku jimbo hilo likiongoza kwa zoezi hilo kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo. 

"Yapo mambo mengi tumeyafanya kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita ambayo hayakuwepo. Niwaombe ndugu zangu mtuchague tena mimi binafsi kuwa mbunge wenu, Mheshimiwa Rais Magufuli na madiwani ili tukatekeleze shughuli za maendeleo kutoka pale tulipoishia,"amesema.

Mgombea Ubunge huyo ameahidi kuendeleza michezo kwa wananchi hao kupitia mashindano aliyokuwa akiyaendesha ndani ya jimbo hilo yanayojulikana kama ‘The Angeline Ilemela Jimbo Cup’  huku akiwasisitiza kutouza viwanja kiholela na kutokacha zoezi la umilikishaji kwa faida yao binafsi na vizazi vyao.

Akimkaribisha mgombea ubunge huyo, Meneja Kampeni wa Jimbo la Ilemela, Ndugu Kazungu Safari Idebe amewataka wananchi hao kuwapuuza wanasiasa wasiokuwa na nia njema wanaohubiri chuki, utengano na kukwamisha maendeleo kwani CCM kupitia mgombea wake wa urais, Dkt John Magufuli na Serikali yake wametekeleza shughuli kubwa ya kuwaletea watanzania maendeleo ikiwemo ukamilishaji wa miradi ya reli ya kisasa, mradi wa umeme wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, ununuzi wa ndege, ujenzi wa hospitali, zahanati na vituo vya afya.

Wakati Mwenyekiti wa chama hicho wilaya ya Ilemela, Nelson Mesha akiwaomba wananchi hao kukiunga mkono chama chake na wagombea wake kwani wamebeba Ilani yenye dira na maono ya Tanzania wanayoitaka.

Kampeni za mgombea Ubunge wa Jimbo la Ilemela kupitia CCM zitaendelea tena leo katika Kata ya Kitangiri,viwanja vya Mihama jimboni humo.

 

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news