SERIKALI mkoani Mtwara imetoa wito kwa Watanzania kutothubutu kusafiri kuelekea nchi jirani ya Msumbiji bila kuwa na vibali au nyaraka halali zitazowatambulisha utaifa wao na kutumia vivuko rasmi vinavyotambulika ili kuepuka madhara ya kiusalama.
Ni madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na ukiukwaji wa utaratibu na ikiwezekana wasubiri hadi pale hali ya usalama katika taifa hilo itakapoimarika.
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Gelasius Byakanwa ameyasema hayo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari juu ya uwepo wa taarifa zinazodai kuwa, kuna raia wa nchi ya Msumbiji ambao wanakimbilia katika maeneo ya jirani na mpaka wa Tanzania na wengine kushambuliwa.
RC Byakanwa
amesema kuwa, suala la kuwataka kutumia utaratibu huo ni kuimarisha ulinzi wa mipaka na kuendelea kujiridhisha juu ya kumbukumbu
sahihi ya Watanzania waliotoka na kuingia nchini.Pia amesema,kutokana na kukauka kwa maji katika mto Ruvuma mpaka wa Tanzania na Msumbiji unapitika kwa urahisi hata kwa kutembea kwa miguu.
Mbali na hayo Mkuu huyo amekanusha uwepo wa taarifa kuwa machafuko yanayoendelea nchini Msumbiji yanaathiri Tanzania na kueleza kuwa vyombo vya ulinzi na usalama hapa nchini vimejipanga imara kulinda usalama wa mipaka yake huku akiwataka wananchi kuendelea kutoa taarifa kwa mtu au kikundi chochote ambao wanawatilia mashaka.