DC Rajab amesema, ameamua kuifunga skuli hiyo kwa muda baada ya kubaini kuwepo kwa matatizo ikiwemo utaratibu wa uajiri wa walimu ambao wamekuwa wakiajiriwa bila ya kuingia mikataba ya kazi pamoja na skuli hiyo kushindwa kufuata taratibu za uanzishaji wa skuli za maandalizi zilizowekwa na Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar.

Akizungumza ofisini kwake mjini Mahonda jijini Zanzibar na walimu wa skuli hiyo waliofika kwa ajili ya kupeleka malalamiko yao, DC Rajab amesema, Serikali haikatazi jamii kuanzisha skuli, hivyo ni vema kwa wanaoanzisha skuli hizo kuzingatia  taratibu zilizowekwa na wizara husika ili kuepusha migogoro ambayo haina ulazima,

Amesema kuwa, endapo sheria na taratibu zitazingatiwa zitasaidia kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi bila usumbufu.

Pia amesema, kwa mujibu wa sheria za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali ni jukumu la kila skuli kuanzisha kamati ya skuli ili iweze kushirikiana na uongozi wa skuli pindi yanapotokea matatizo kama hayo.

Hata hivyo, DC Rajab amemuagiza Sheha wa Shehiya ya Kiwengwa kumtaarifu mmiliki wa skuli hiyo ndugu Rozana kufika ofsini kwake Mahonda pamoja na walimu hao ili waweze kulizungumza tatizo hilo kwa kina na kulitafutia ufumbuzi ili kila mtu apate haki yake.

Skuli ya maandalizi Amish Marafiki Kiwengwa ni skuli ya binafsi iliyoanzishwa na Mwekezaji Rozana mwaka 2019 jijini Zanzibar.