KUKAMILIKA kwa Mradi wa Kufua Umeme kwa maji wa Julius Nyerere (JNHPP) utakaozalisha jumla ya Megawati 2115, kunatarajiwa kuongeza kasi ya maendeleo na kuwa injini ya ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Utekelezaji wa mradi huu mkubwa na wa kimkakati ulianza mwezi Juni 2019 na unatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2022.Hayo yameelezwa na Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akiwa katika ziara yake kukagua utekelezaji wa mradi huo.
Aidha, kulingana na mpango kazi uliopo, Serikali imeshamlipa Mkandarasi zaidi shilingi trilioni 1.49 ambayo ni sawa na asilimia 22 ya malipo.Mradi wa Julius Nyerere unatekelezwa kwa kutumia fedha za ndani ambacho ni kiasi cha shilingi trilioni 6.558.
Kwa mujibu wa Dkt. Kalemani mradi wa JNHPP utakuwa injini ya uchumi wa Tanzania, kwani kukamilika kwake kunatarajiwa kushusha bei ya umeme na kukuza uwekezaji hasa sekta ya viwanda nchini.
Mradi huu pia, utasaidia kuhifadhi mazingira na kupunguza ukataji wa miti kutokana na kushuka kwa gharama za umeme.
"Lengo la Serikali ni kuhakikisha mradi wa Julius Nyerere unakamilika ndani ya wakati,"amesema Dkt. Kalemani.Ameongeza kuwa, mradi wa JNHPP ndio utakaotatua matatizo ya umeme nchini hivyo kukamilika kwake kuna tija kubwa sana kwa Taifa.Katika ziara hiyo, Dkt. Kalemani aliambatana Naibu Waziri wa Ujenzi Misri Mhandisi Jenerali Mohmoud Nassar, Katibu Mkuu Nishati Mhandisi Zena Said, Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Edward Ishengoma, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TANESCO Dkt. Alexander Kyaruzi, Mkurugenzi Mtendaji TANESCO Dkt. Tito Mwinuka na Naibu Mkurugenzi Uwekezaji TANESCO Mhandisi Khalid James.
Siku zahesabika Tanzania kuandika historia kupitia JNHPP, mradi unaotajwa kuwa injini ya ukuaji uchumi nchini
Tags
Uchumi