NA MWANDISHI MAALUM
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan leo Novemba 10, 2021 amewasili mjini Cairo nchini Misri kuanza ziara ya Kiserikali ya siku tatu.
Mapema alipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Cairo, Mhe. Rais Samia amepokelewa na Waziri wa Nchi anayeshughulikia Uhamiaji na Wamisri Waishio Nje, Mhe. Nabila Makram.



Mara baada ya kuwasili Ikulu mjini Cairo, Mhe. Rais Samia amefanya mazungumzo rasmi na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mhe. Abdel Fattah Al-Sis na kuzungumza na waandishi wa habari ambapo mazungumzo hayo yamezungumzia maeneo kadhaa ya ushirikiano wa pamoja katika nyanja za elimu, nishati, michezo, ulinzi na ushirikiano wa kijeshi pamoja na umuhimu wa kuendeleza Tume ya Pamoja ya Ushirikiano iliyoanzishwa mwaka 1989.
Mhe. Rais Samia amempongeza Rais Al- Sisi na Serikali yake kwa kuamua kuanza kufundisha lugha ya Kiswahili katika taasisi za elimu ya juu nchini Misri kama lugha ya kimkakati na kumuahidi kutuma timu ya wataalam kutoka Tanzania kuisaidia Misri katika kufanikisha lengo lake hilo.
Aidha, Mhe. Rais Samia pia amemshukuru Rais Al-Sisi kwa ushirikiano uliopo wa kijeshi ambapo wataalam wengi kutoka Tanzania wameendelea kupata mafunzo mbali mbali ya kijeshi nchini Misri.
Mhe. Rais Samia pia amezungumza na mwenyeji wake juu ya umuhimu wa kushirikiana pamoja katika kuhakikisha changamoto zote zilizopo katika ujenzi wa Mradi wa Umeme wa Mwalimu Nyerere zinaondolewa ili kukamilisha mradi huo wa kimkakati ambao unatekelezwa na kampuni za Misri.
Viongozi hao wawili pia wamezungumzia umuhimu wa kuongeza fursa za biashara na uwekezaji kati ya Misri na Tanzania ambapo kwa hivi sasa biashara baina ya nchi hizo mbili imeongezeka kutoka Shilingi Bilioni 84.3 mwaka 2018 hadi kufikia Shilingi Bilioni 87.3 mwaka 2020.
Aidha, Mhe. Rais Samia amesema Misri imewekeza nchini Tanzania katika miradi 26 yenye thamani ya kiasi cha Shilingi Trilioni 3.1 na kutengeneza ajira 2,206 kwa watanzania.
Marais hao wawili wameshuhudia utiaji saini wa Hati tatu za makubaliano katika nyanja za michezo, elimu na elimu ya juu.