NA FRESHA KINASA
KADA wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Musoma Mjini, Mwalimu Makuru Lameck Joseph amesema mawaziri, makatibu wakuu na manaibu katibu wakuu walioteuliwa na Rais Samia Suluhu Hassan wanawajibu wa kufanya kazi kwa kuzingatia shabaha ya teuzi zao katika kukidhi malengo ya Rais aliyewaamini kuwateua wamsaidie kusukuma mbele gurudumu la maendeleo kwa Watanzania.
Mwalimu Makuru amesema, hatua ya Rais Samia Suluhu Hassan kuwaamini na kuwateua ameona kuwa wana uwezo mzuri wa kumsaidia kutatua kero mbalimbali za wananchi na kushiriki kikamilifu katika ajenda ya kuliletea maendeleo Taifa. Hivyo watumie vyema nafasi zao kuwatumikia wananchi kwa uadilifu, upendo, juhudi na kwa moyo thabiti.
Ameyasema hayo wakati akizungumza na DIRAMAKINI BLOG Mjini Musoma ambapo pamoja na mambo mengine amewapongeza kwa kuteuliwa kwao na kusema kuwa kila mtanzania anapaswa kuwaombea na kuwapa ushirikiano wa dhati katika safari yao ya kuwatumikia wananchi.
Ameongeza kuwa,Taifa lina hazina kubwa ya viongozi ambao hawajapata nafasi ya kuteuliwa, lakini wana uwezo mkubwa wa kuwatumikia watanzania na kuwaletea maendeleo.
Hivyo viongozi walioteuliwa wamshukuru Rais Samia na kudra za Mwenyezi Mungu kwa kuwapa kibali cha kuwatumikia watanzania wasijisahau hata kidogo kwa kutowajibika kikamilifu kutatua matatizo nankero za wananchi hatua ambayo inaweza ikamvunja Rais moyo.
"Wanawajibu wa kuwajibika kufanya kazi kwa weledi na kwa kufuata sheria za nchi pasipo kuwakandamiza na kuwaonea wananchi. Wajikite katika ajenda za kuleta maendeleo kwa wananchi wakimsaidia Rais pasipo kupendelea, kubagua mtu yeyote ama kumuomea mtu bali watende haki kama sheria na miongozo ya nchi inavyotaka na kwa kuzingatia viapo vyao walivyoaapa baada ya kuapishwa,"amesema Mwalimu Makuru.
Pia, amewaasa waache makundi, majungu, fitina, unafiki na kujipendekeza kwani hayo yote ni adui wa haki na ni vikwazo vya maendeleo katika Taifa ambavyo hatimaye huleta sintofahamu kwa wananchi na migawanyiko ambayo nadni yake huleta chuki miongoni mwa wananchi na viongozi wanaowaongoza.
Katika hatua nyingine, Mwalimu Makuru amewaomba Watanzania wote waendelee kumuamini Rais Samia Suluhu Hassan kwani shabaha yake iko wazi kwa Watanzania kuwafikisha mahali pazuri sana kimaendeleo.
Tags
Habari
Binafsi nawaombea sana lkn pia nakuombea wewe upate mpenyo kwani nayakubali mawazo yako na ninaona uelekeo mzuri kwako. Mungu akubariki na akutangulie.
ReplyDelete