NA DIRAMAKINI
TIMU ya taifa ya wasichana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Girls imefanikiwa kusonga mbele Raundi ya mwisho ya mchujo wa kuwania tiketi ya Kombe la Dunia baadaye mwaka huu India licha ya kuchapwa 2-1 na Burundi jana Uwanja wa Amaan jijini Zanzibar.

Awali Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe, Mohamed Mchengerwa aliwatakia kila la heri wachezaji wa Taifa ya wanawake U 17 ya Serengeti Girls kufanya vizuri kwenye mechi ya kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Burundi.
Mhe. Mchengerwa alizungumza na wachezaji wa Serengeti muda mfupi kabla ya kuanza kwa mechi hiyo ambapo amesema Rais Samia Suluhu Hassan ana matarajio makubwa na timu hiyo.
Alisema kuwa, anatambua kuwa timu hiyo ilipata ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Burundi mjini Kigali lakini isibweteke na badala yake itoke na ushindi wa kishindo ili kuwaogopesha Cameroon.
Ameahidi kuwa baada ya mechi hii atakwenda kuwaona na kuwashukuru kwa niaba ya Mhe. Rais na kuandaa chakula cha pamoja.
"Ni matarajio yetu kuwa timu ya Serengeti ikifuzu tutakuwa tumeziingiza timu mbili kwenye mashindano ya kombe la Dunia baada ya timu ya soka ya walemavu ya Tembo Warriors,"amesema.
Amesisitiza kuwa baada ya ushindi wa leo Serikali itaendelea kutoa kila msaada unaotakiwa ili timu izidi kufanya vizuri zaidi.