NA MWANDISHI WETU
SERIKALI imesema inaboresha vituo vya walimu kwa lengo la kuendelea kutoa fursa kwa walimu kupata mafunzo wakiwa kazini ili kuwajengea uzoefu.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Mhe.Prof.Adolf Mkenda, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia wakati wa semina ya utambulishaji wa mjadala wa wazi juu ya kitabu cha wasifu wa Mwalimu Julius Nyerere ambapo kumekuwa na mazungumzo juu ya ubora wa elimu na ndio maana maboresho hayo yanafanyika ili kuhakikisha elimu inayotolewa inakuwa bora, lakini pia inahakisi hali halisi ya maisha.

Waziri Mkenda ametumia fursa hiyo kuwaomba wadau kuendelea kutoa maoni ya kuboresha mitaala na kwamba kwa kuwa sheria ya elimu nayo itafanyiwa mapitio itasaidia kupunguza mabadiliko ya mara kwa mara kwenye elimu yanayotokana na mabadilko ya viongozi wa elimu.

Naye Mkurugenzi Mkuu Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia, Dkt. Amos Nungu amesema atahakikisha juzuu hizo zinatafsiriwa ikiwa ni pamoja na kurejesha Kavazi ya Mwalimu.

Akizungumza katika mjadala huo, Mwalimu mstaafu Fauster Sokiri amesema usalama wa nchi hii unategemea pamoja na mambo mengine Wizara ya Elimu hivyo ni vizuri kuendelea kufanya maboresho ya sifa za kuajiri walimu kwa lengo la kuendelea kuboresha elimu.