NA VERONICA MWAFISI
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama ametoa wito kwa wananchi wa Vijiji vya Karangai na Maweni, Halmashauri ya Wilaya ya Meru kutumia hatimiliki za kimila walizonazo kufanya shughuli za maendeleo ili kujikwamua kiuchumi.
Mhe. Jenista ametoa wito huo mara baada ya kukagua na kuzindua masijali za ardhi za Vijiji vya Karangai na Maweni katika Halmashauri ya Wilaya ya Meru mkoani Arusha zilizojengwa na Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA).
Mhe. Jenista amesema MKURABITA imekuwa ikifanya kazi nzuri ya kurasimisha ardhi, lengo likiwa ni kuwasaidia wananchi kufanya shughuli za maendeleo na kujikwamua kiuchumi.

“Kitendo cha MKURABITA kupima na kukabidhi hatimiliki za kimila, tayari imeshakuondolea umaskini, hivyo ni namna sasa ya wewe uliyenufaika na hatimiliki hiyo kufuata maelekezo ya kuitumia kwa maendeleo yako kwani hati hiyo ni dhamana yako ya kupata mkopo,” Mhe. Jenista amesisitiza
Mhe Jenista amewasisitiza wananchi hao kutoogopa kukopa fedha kwa ajili ya kufanya shughuli za maendeleo kwani mtu akitaka kuwa na maendeleo hawezi kuepuka kukopa.

“Msigope kukopa kwani mikopo ndiyo inayowasaidia wengi kuinuka kiuchumi na ndio maana Serikali imewarasimishia ardhi ili mpate hati ambazo zitawasaidia kukopa na kufanya shughuli za maendeleo ili lengo la serikali la kuona uchumi wa mtu mmoja mmoja unakua linafikiwa.,”Mhe. Jenista ameongeza.
Katika kuwawezesha wananchi hao kukopa, Mhe.Jenista ameziomba taasisi za kifedha kuitikia wito wa serikali wa kushusha riba hadi kufikia digitali moja.
Aidha, Mhe. Jenista amewataka watumishi wa masijali za ardhi alizozizindua kutenda haki katika kuwahudumia wananchi.
“Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kupitia MKURABITA amewajengea ofisi nzuri hivyo mtumie ofisi hizo kuwahudumia wananchi kwa kutenda haki, utendaji wenu wa kazi uwe tofauti na wengine,” Mhe. Jenista amesisitiza na kuongeza kuwa shughuli zote zifanyike kwa uwazi ili kutoipa rushwa nafasi.
Kwa upande wake, Mratibu wa MKURABITA, Dkt. Seraphia Mgembe amewasisitiza wananchi wa vijiji hivyo kutumia masijala zilizozinduliwa kufanya shughuli za maendeleo.
“Lengo la kujengwa kwa masijala hizi ni kufanya shughuli za maendeleo na sio vinginevyo, hivyo mzitumie vizuri ili kuhakikisha maendeleo ya mmoja mmoja na taifa kwa ujumla yanapatikana,” Dkt. Mgembe amesisitiza.
Mhe. Jenista yuko mkoani Arusha kwa ziara ya kikazi ambapo pamoja na kuzindua masijala katika Vijiji vya Karangai na Meru katika Halmashauri ya Wilaya ya Meru, alizindua pia Kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara na katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha.