NA OR-TAMISEMI
WAGANGA wakuu wa halmashauri zote nchini wamehimizwa kuhamasisha utolewaji wa matone ya Vitamin A kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano.

Rai hiyo imetolewa Februari Mosi, 2023 na Afisa Lishe kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI), Bi.Asiatu Mbwambo wakati wa kikao kazi cha timu ya usimamizi shirikishi kutoka OR-TAMISEMI na watoa huduma wa kituo cha afya Matemanga kilichopo wilayani Tunduru.

"Watoto wanatakiwa kula vyakula mchanganyiko, lakini milo yetu haikidhi aina ya vyakula kutoka makundi matano ya vyakula kwa hiyo matone ya Vitamin A yana vitamins zinazosaidia kuboresha afya na kuimarisha ukuaji wa mtoto.

Amesema kuwa, utolewaji wa matone ya Vitamin A kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano ni moja ya mikakati ya Serikali ya kuboresha afya za watoto baada ya tafiti kuonesha kwamba upungufu wa Vitamin A kwa watoto huchangiwa pia na ulaji duni.
Mbwambo alitumia fursa hiyo kutoa wito kwa wazazi na walezi wote wenye watoto walio chini ya miaka mitano kuhakikisha wanawapeleka watoto kupata matone ya Vitamin A katika kampeni zinazofanyika kila mwezi Juni na Desemba nchi nzima.