NA MWANDISHI WETU
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulika na Sera Bunge na Uratibu, Mhe. Jenista Mhagama amesema, Serikali imeridhia kuwa na kifungu maalumu cha bajeti kwa ajili ya kuendesha Baraza la Vyama Vya Siasa ili kuweza kufanya shughuli zake kwa ufanisi.

Hayo ameyabainisha leo Aprili 16, 2023 wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Baraza la Vyama Vya Siasa kilichofanyika jijini Dar es Salaam.
Mheshimiwa Waziri amesema,Serikali imepitisha bajeti ya shilingi billioni 1,586,662,000.00 kwa ajili ya kuendesha Baraza la Vyama Vya Siasa kwa mwaka wa fedha 2023/24.

Ameongeza kuwa, Baraza la Vyama vya Siasa lipewe nafasi ya kukutana na Serikali ili kujadiliana kuhusu mambo mabalimbali yanayohusu ustawi wa demokrasia nchini.
"Iko miradi ya kimkakati hapa nchini, kuna kila sababu viongozi wa vyama vya siasa na Baraza la Vyama vya Siasa wapate nafasi ya kuangalia miradi hiyo, kwa sababu tunapofika kwenye masuala ya maendeleo ya nchi na ustawi nchi hakuna chama.
“Kuna nafasi ya viongozi wa vyama vya siasa kutushauri vizuri zaidi kwa ustawi wa wananchi,"amesema Waziri Mhagama.

Pia amesema, "tunahitaji kutengeneza programu maalumu ya mafunzo kwa ajili ya viongozi wetu wa vyama vya siasa, ili tuendelee kuimarisha demokrasia ya vyama vingi nchini, hatuwezi kufanikiwa kama viongozi wetu hawataendana na mabadiliko yanayoyendelea kwenye ulimwengu wa sasa."
Katika hatua nyingine, Waziri Mhagama ameomba migogoro ya vyama imalizwe ndani ya vyama, "tuna uwezo wa kuimaliza sisi wenyewe, tujenge uwezo wa kutizama matatizo yetu ndani ya chama na kuyamaliza ndani ya vyama vyetu."
Waziri amehimiza viongozi wa vyama vya siasa, kuzingatia sheria za matumizi na mapato ya fedha.
Waziri Mhagama ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha mfumo wa vyama vingi nchini Tanzania.

“Mhe. Rais alipoingia madarakani aliasisi ”4r” ambazo ni (reconciliation, resilience, reform and rebuilding) kwa Kiswahili ni maridhiano, ustahimilivu, mageuzi na mabadiliko hii ikiwa ni kwa lengo la kutoa mwongozo wa jinsi ambavyo siasa za nchi yetu zinapaswa kuwa.”
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Vyama Siasa, Juma Ally Khatibu, ameomba mfaunzo ya siku tatu mara tu baada ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani ili kuwa na uelewa mkubwa kuhusu ”4r”.
Mafanikio ya Kikosi kazi katika Mkutano ule uliofunguliwa na Mhe. Dkt, Samia Suluhu Hassan jijini Dodoma ambao ni zao la Baraza la Vyama Vya Siasa, ni pamoja na kufanyika kwa mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa, mafanikio mengine ni kuundwa kwa Tume ya Rais ya kuangalia namna ya kuboresha Taasisi za Haki Jinai nchini.