DAR ES SALAAM-Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA), Joel Laurent amewataka watumishi wa Mamlaka kutanguliza maslahi ya Taifa kabla ya maslahi yao binafsi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

"Tunapofanya kazi zetu tufikirie zaidi tunaitendea nini taasisi kabla ya kufikiria kuwa taasisi inakutendea nini?" Laurent alisisitiza.
Mkurugenzi Laurent aliongeza kuwa, utekelezaji wa majukumu ya Mamlaka ni utekelezaji wa maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Ameongeza kuwa, maono hayo ni pamoja na kuhakikisha mbolea bora inapatikana kwa wakulima wote kwa wakati.
Laurent ameeleza hayo mwishoni mwa wiki wakati wa kutaniko la watumishi wa Mamlaka lililolenga kutoa mafunzo katika eneo la afya, kujenga umoja (team building) pamoja na kushiriki katika michezo mbalimbali kwa ajili ya kuimarisha afya za watumishi na kufahamiana.
Aidha, amewataka watumishi kujiuliza endapo wana weledi wa kutosha katika kutekeleza majukumu yao na kuwataka waongeze juhudi ya kutafuta maarifa yanayokosekana ili kuongeza tija katika utendaji wao pindi wanapobaini wamepungukiwa na ujuzi.
"Kabla hujafanya kazi kwa weledi ujue majukumu yako kwa weledi, kama umebaini huna weledi bainisha eneo lenye changamoto na kuwasilisha utawala ili uwekwe kwenye mpango wa mafunzo uendelezwe,"Laurent alikazia.

Akizungumza wakati wa kutaniko hilo, Mkurugenzi wa Huduma za Mamlaka, Victoria Elangwa ameeleza kuwa, watumishi hao wamepewa mafunzo ya ufahamu juu ya magonjwa mbalimbali ikiwa ni pamoja na UKIMWI, MSY, na saratani pamoja na namna ya kukabiliana na msongo wa mawazo.
Aidha, ameeleza kuwa watumishi wamepata fursa ya kupima afya zao ikiwa ni pamoja na kujua uwiano wa urefu na uzito wao (BMI) na kushauriwa ipasavyo, kupima endapo wana athari katika eneo la tezi dume kwa wanaume, saratani ya shingo ya kizazi kwa wanawake, homa ya ini pamoja na kupata fursa ya kuchanja chanjo ya homa ya ini.

Akizungumza kwa niaba ya watumishi wa Mamlaka, Meneja wa kitengo cha Rasilimali watu na Utawala, Naomi Fwemula amewasihi watumishi kuzingatia yote yaliyofundishwa kwa siku mbili kunzia tarehe 1-2, Desemba ili yatufae siku kwa siku.
Aliwaomba kuendelea kushirikiana kujituma na kuwa wabunifu katika utendaji kazi wao ili kuonesha uhai wa taasisi.