DODOMA-Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi wametakiwa kuchagua Viongozi bora wenye weledi wa kusimamia maslahi ya Wafanyakazi na wanaoweza kuendesha Baraza kwa tija.
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Jumanne Sagini (Mb), akizungumza wakati akifungua Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Wizara hiyo kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Meja Gen. Mzee uliopo Makao Makuu ya Jeshi la Magereza Msalato Jijini Dodoma, tarehe 16 Januari, 2024.
Hayo yamesemwa Januari 16, 2024 na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Jumanne Sagini (Mb) wakati alipokuwa akifungua Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi katika Ukumbi wa Mikutano wa Meja Gen. Mzee uliopo Makao Makuu ya Jeshi la Magereza Msalato Jijini Dodoma na kuwataka wajumbe kuchagua Viongozi wa kusimamia maslahi ya wafanyakazi.
"Baraza hili ni chombo muhimu cha kuushauri Uongozi wa Wizara kuhusu masuala mbalimbali ya maslahi ya Wafanyakazi na upangaji wa mipango, bajeti na utekelezaji wake kwa ujumla hivyo basi ni muhimu kwa wajumbe kutafakari na kuchagua Viongozi bora wenye uwezo na weledi wa kusimamia maslahi ya wafanyakazi na kuepuka kuchagua kwa mihemuko na uanaharakati".
"Nami kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Mhandisi Hamad Masauni (Mb) tunaahidi kushirikiana bega kwa bega na Wajumbe wa Baraza hili ili kuhakikisha Wizara yetu inafikia kiwango cha juu katika kutekeleza majukumu tuliyokabidhiwa,"alisema Mhe. Sagini.
Aidha, Mhe. Sagini alimpongeza Rais wa Awamu ya Sita ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuboresha Utumishi wa Umma na kushughulikia maslahi na stahiki mbalimbali za Wafanyakazi zikiwemo kulipa Madeni ya Watumishi, Kupandisha Madaraja, kupandisha vyeo Wafanyakazi na kulipa mafao ya watumishi waliostaafu utumishi wa Umma kwa mujibu wa sheria za Nchi, Mhe. Rais amelipa areas ya malimbikizo ya mishahara, ameajiri watumishi wapya.
Hata hivyo, Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Wizara ya Mambo ya Ndani linafanyika ikiwa ni utekelezaji wa Agizo Na. 1 la mwaka 1970 la Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linalosisitiza Waajiri kuunda Mabaraza mahala pakazi, lengo kuu likiwa ni kuwashirikisha Wafanyakazi kujadili mipango ya kazi, bajeti na utekelezaji wa mipango waliyojiwekea kwa pamoja.
Awali Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Wafanyakazi ambaye ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Kaspar Kaspar Mmuya, alitoa salamu za Wafanyakazi wa Wizara hiyo pamoja na Idara zake kwa Mgeni Rasmi na kumueleza kuwa wapo tayari kupokea maelekezo atakayoyatoa katika kikao hicho na kwenda kuyafanyia kazi.