NHC yanunua rasmi eneo la Urafiki

DAR-Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limenunua rasmi eneo la Urafiki na majengo yaliyokuwa chini ya Kampuni ya Urafiki wa Tanzania na China (Tanzania - China Friendship Textile CO LTD). 
Meneja wa Mawasiliano kwa Umma wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Muungano Saguya ameyasema hayo leo wakati wa ziara ya kukagua maeneo mbalimbali ambayo sasa yatakuwa chini ya miliki ya NHC na kufafanua kuwa eneo hili linajumuisha nyumba, maghala, viwanja vya wazi, viwanda na mali nyinginezo.

Katika ziara yake, Saguya alielezea furaha yake na matumaini makubwa kuhusu hatua hii, akibainisha kwamba itasaidia kuboresha miundombinu na kuinua uchumi wa maeneo hayo na kuboresha mandhari ya jiji.

Amesema kuwa, NHC imelinunua eneo hilo lenye ukubwa wa zaidi ya ekari 50 kutoka kwa mnada wa wazi likiwa na thamani ya zaidi ya shilingi bilioni tatu.

"Kupitia umiliki huu mpya, Shirika la Nyumba la Taifa limejipanga kuboresha maeneo haya ili kuendana na malengo yetu ya kutoa makazi bora na ya kisasa kwa wananchi. Tumeanza kwa kulipima eneo lote na kutambua mipaka yote inayolihusisha eneo hilo."
Eneo la Urafiki lina historia ndefu ya kuwa kituo muhimu cha viwanda na makazi, kikitoa mchango mkubwa katika uchumi wa Tanzania.

Hivi sasa, NHC inapanga kufanyia maboresho makubwa eneo hili kwa kujenga miundombinu bora, nyumba za kisasa, na maeneo ya biashara ambayo yatavutia wawekezaji na wakazi wapya.

Shirika la Nyumba la Taifa linaamini kuwa mradi huu mpya utakuwa na manufaa makubwa kwa taifa kwa ujumla, na kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya makazi na maendeleo ya kiuchumi nchini.
Katika mpango wa maendeleo ya NHC, eneo la Urafiki litawekewa mkazo maalum kwa ajili ya kuhakikisha kuwa linakuwa mfano bora wa maendeleo ya kisasa na endelevu.

Muungano alihitimisha kwa kusema, "Hii ni hatua muhimu kwa NHC na kwa taifa letu. Tunawaomba wananchi na wadau mbalimbali kuunga mkono juhudi zetu katika kuboresha na kuendeleza maeneo haya kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Wabia wakuu wa kiwanda hicho ni Msajili wa Hazina na kampuni Kampuni ya Urafiki wa Tanzania na China (Tanzania - China Friendship Textile CO LTD). Kiwanda hicho ni matokeo ya urafiki wa China na Tanzania na kina historia ndefu na mahusiano ya muda mrefu.

Kabla ya hapo kumekuwa na mvutano mkubwa baina ya kampuni iliyokuwa inamiliki kiwanda hicho na wafanyakazi jambo lililokuwa limewafikisha katika hatua mbalimbali za masuluhisho mpaka pale kiwanda hicho kilipopigwa mnada ili kuweza kuokoa mali za Kampuni.Hayo yamejitokeza wakati wa ziara ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa ( NHC), Hamad Abdallah, akiwa kwenye ziara ya kutembelea miradi inayotekelezwa na NHC Jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kukagua na kuona maendeleo yake.

Hamad amefanya ziara katika miradi ya Samia Housing, Morocco Square, Shule ya Uchumi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na eneo la Urafiki jijini Dar es Salaam.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news