Serikali kuwapatia vijana maeneo ya uchimbaji ikiwa ni suluhu ya uvamizi migodini

MARA-Katika kuhakikisha inakabiliana na changamoto ya uvamizi kwenye migodi mikubwa, Serikali imepanga kutenga maeneo ya uchimbaji na kuwapatia vijana ili wawe na sehemu ya kujipatia kipato.
Hayo yalibainishwa Mei 30, 2024 na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde alipofanya ziara ya kikazi na kuzungumza na wananchi wanaozunguka Mgodi wa North Mara katika eneo la Nyamongo wilayani Tarime.
“Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameagiza kuwa hataki kuona vijana wanahangaika na kujihusisha na uvamizi migodini kwa kukosa maeneo ya uchimbaji. Wizara ya Madini tumeweka mkakati kupitia maeneo ambayo yamerudi Serikalini baada ya kufutwa leseni, tunakwenda kutenga maeneo mahsusi kwa ajili ya kuwapatia vijana wachimbe madini na kuendesha maisha yao” alisema Waziri Mavunde.
Alisema kwamba, ni dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuhakikisha vijana wanapewa kipaumbele katika fursa zilizopo kwenye madini na kuongeza,

“Serikali haifurahii hata kidogo uvamizi na migogoro mbalimbali inayojitokeza baina ya migodi na wananchi wanaozunguka maeneo ya migodi hiyo."
Pia, Waziri Mavunde alibainisha kuwa tayari Wizara imefanya mazungumzo na Kampuni ya Barrick ili katika leseni zao za utafiti walizonazo katika maeneo ya Nyamongo, waweze kutenga eneo kwa ajili ya kuwapatia wachimbaji wadogo ikiwa ni pamoja na kufanya utafiti wa awali wa kusaidia wachimbaji hao.

Vilevile, Waziri Mavunde aliahidi kulielekeza Shirika la Madini la Taifa ( STAMICO) liweze kupeleka mitambo Nyamongo katika maeneo ya wachimbaji wadogo yatakayotengwa kwa ajili ya kusaidia kuchoronga ili kuongeza tija kwenye uchimbaji wao.Awali, akitoa ufafanuzi kuhusu uvamizi migodini, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Mhandisi Hamad Masauni alitoa wito kwa Jeshi la Polisi kuendelea kutoa elimu kwa wananchi na kuwataka Askari Polisi kuwa rafiki na jamii kwa ajili ya ulinzi wao na mali zao.
Akitoa salamu za wananchi wake, Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini, Mhe. Mwita Waitara alipongeza jitihada mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali katika kutatua kero na changamoto za eneo la Nyamongo, na kuwaomba wananchi kuendelea kuiamini Serikali yao kwa kuwa inaendelea kuwapelekea ya kweli.
Naye, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Mhe. Kanali Evans Mtambi aliwashukuru Mawaziri kwa kufika uwandani kutatua changamoto za wananchi na kuahidi kuendelea kusimamia maelekezo yote waliyotoa ili kuboresha maisha ya wananchi kwenye maeneo yanayozunguka migodi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news