Waziri Mkuu atoa wito kwa wanaotekeleza afua za wanawake

MWANZA-Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa wito kwa wadau wanaotekeleza afua mbalimbali za wanawake watumie taarifa na takwimu za sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 katika kuandaa mipango na mikakati ya uwezeshaji wa wanawake nchini.Mbali na hayo pia Mheshimiwa Majaliwa amewasisitiza wadau hao wanaotekeleza afua za wanawake waandae mipango yao kwa kuzingatia vipaumbele vya Serikali. “Hii ni namna bora ya kuharakisha ustawi na maendeleo ya wanawake.”

Mheshimiwa Majaliwa ameyasema hayo Jumamosi, Mei 18, 2024 katika hafla ya utoaji wa tuzo ya Malkia wa Nguvu iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Kwa Tunza Beach jijini Mwanza.
Pia, Waziri Mkuu amesema kuanzia Julai 2024 Serikali itatoa utaratibu wa namna ya uendeshaji na utoaji wa mikopo kwa makundi ya wanawake, vijana na wenye ulemavu ili kuwawezesha kujikwamua kiuchumi.

“Nitoe rai kwa wanawake wote na makundi ya vijana na watu wenye ulemavu wazingatie utaratibu utakaotolewa na niwakumbushe kuwa fedha inayotolewa ni mikopo siyo ufadhili hivyo wanufaika wote wawajibike kuirejesha.”

Waziri Mkuu amesema, Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kutoa kipaumbele katika masuala ya uwezeshaji wa kiuchumi kwa makundi maalum ya wanajamii likiwemo kundi la wanawake.
Amesema, Serikali kwa mwaka 2023/2024 imetenga kiasi cha shilingi bilioni 18.5 kwa ajili ya kutoa mikopo hiyo kwa riba ya asilimia saba na kufanya makubaliano na NMB yatakayowezesha wafanyabiashara ndogondogo wakiwemo wanawake kupata mikopo yenye riba nafuu.

“Ninafuraha sana kwa kuwa hamasa inayotokana na ushiriki wa Tuzo ya Malkia wa Nguvu imeendelea kuwavuta wanawake wengi zaidi na kuwafanya waongeze ubora wa shughuli wanazozifanya sambamba na kukuza biashara zao.”
Amesema anafahamu kuwa moja ya malengo ya Mradi wa Malkia wa Nguvu ni kuimarisha fursa za ajira na kuwa kichocheo muhimu cha uzalishaji wa ajira mpya. “Ninawapongeza sana kwa kuchangia jitihada za Serikali katika kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana.”

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news