Hati safi zaing’arisha Kasulu

NA RESPICE SWETU

MKUU wa Mkoa wa Kigoma, Thobias Andengenye ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu kwa kupata hati safi katika ukaguzi wa fedha na hesabu za serikali uliofanyika kwa kipindi cha miaka minne mfululizo. Pongezi hizo amezitoa wakati wa kikao maalumu cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu kilichokutana kujadili taarifa hiyo.

Akisoma taarifa hiyo kwenye kikao cha baraza la madiwani, Mweka Hazina wa Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu, Sarah Kibona amesema,kwa kipindi cha miaka minne, Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu imepata hati safi.

Taarifa hiyo imebainisha kuwa, katika ukaguzi wa mdhibiti mkuu wa fedha na hesabu za serikali uliofanyika mwaka wa fedha wa 2019/2020, 2020/2021, 2021/2022 na 2022/2023 halmashauri ya wilaya ya Kasulu ilipata hati safi.

Kufuatia taarifa hiyo,Mkuu wa Mkoa wa Kigoma aliyekuwa mgeni rasmi katika kikao hicho, ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu kwa mafanikio hayo na kuwataka watendaji na madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Kasulu, kuyalinda mafanikio hayo.
Amesema, Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu inatakiwa kuhakikisha kuwa hakuna hoja zitakazokuwa zinajirudia wakati wa ukaguzi ujao, kufungwa kwa hoja zilizopo na kuzidisha umakini wakati wa zoezi la kujibu hoja hizo.

Aidha mkuu wa mkoa wa Kigoma amewataka wakuu wa idara na vitengo kulipa umuhimu suala hilo kwa kushirikiana na kushiriki kikamilifu katika kujibu hoja hizo badala ya kukaimisha jukumu hilo kwa watu wengine au kuwaachia waidizi wao.

Maelekezo mengine aliyoyatoa Andengenye wakati wa kikao hicho ni kukamilisha majibu ya hoja za nyuma na kutekeleza maagizo yaliyotolewa katika kikao cha tawala za mikoa na serikali za mitaa LAAC.

“Ukaguzi unaofanyika ni muhimu na ni matakwa ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ukaguzi huu unafanywa na watu waungwana sana hatupaswi kuwaona ni maadui bali tuwaone kuwa ni marafiki zetu na kushirikiana.

“Ni matumaini ya serikali kuwa, kufikia mwaka wa fedha wa 2025/2026 idadi ya hoja zitapungua na kufikia tarakimu moja kuliko vilivyo sasa,”ameongeza.

Awali akimkaribisha mkuu wa mkoa kuzungumza na wajumbe wa kikao hicho, katibu tawala wa mkoa wa Kigoma Hassan Lugwa, amewaahidi madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Kasulu kuwaletea wataalamu watakaowapa mafunzo kuhusu ukaguzi wa hoja hizo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news