Dira ya Taifa 2050 ni maono ya nchi siku za usoni-Dkt.Biteko

MWANZA-Imeelezwa kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo ni picha na maono kuhusu mustakabali tarajiwa wa maendeleo ya nchi kwa siku za usoni.
Hayo yamebainishwa leo Julai 20, 2024 na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko wakati akifungua Kongamano la Kwanza la Kikanda kuhusu Maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 jijini Mwanza.
"Maandalizi ya Dira ni sehemu ya upangaji maendeleo na sisi kama Taifa ili tuweze kustawi hatuna budi kuchukua hatua madhubuti za kuchochea maendeleo ili kufikia kiwango tarajiwa katika siku za usoni.

Pia, kongamano ni sehemu ya zoezi la ushirikishaji wadau na ukusanyaji maoni ya Dira na makongamano kama hayo na mbinu nyingine zinazotumika kukusanya maoni ya wadau (mfano simu za mkononi, tovuti na mahojiano ya ana kwa ana katika ngazi ya kaya.

Ameongeza kuwa, kupitia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, Tanzania imeweza kupiga hatua kubwa ikiwemo kuingia kwenye orodha ya nchi ya uchumi wa kipato cha kati cha chini (lower middle-income country) mwaka 2020 baada ya kufikisha wastani wa kipato cha mtu cha dola za kimarekani 1,080.
"Ukiacha kipato na kiwango cha jumla cha maendeleo ya watu, Tanzania bado iko nyuma katika vipimo mbalimbali vya maendeleo ukilinganisha na viwango vya kimataifa pamoja na nchi nyingine zilizo katika kundi la uchumi wa kipato cha kati (middle-income countries)," ameongeza Dkt. Biteko.

Aidha, maandalizi ya Dira 2050 yanapaswa kulazimisha kuungalia uhalisia ili kuuliza maswali pamoja na kudadavua ni sababu zipi zimepeleka kuwa katika hali iliyopo sasa na ni kwa namna gani kujikwamua ili kufikia viwango vya juu vya kipato pamoja na ustawi wa maendeleo ya binadamu.
Dkt. Biteko amesema kuwa, Serikali imeamua kufanya makongamano ya kikanda ili kupata maoni ya wananchi na wadau wengi zaidi hivyo, kongamano hili si mwisho bali mwanzo wa makongamano mengine yatakayofanyika kwa kushirikisha mikoa ya nchi nzima katika mikoa ya Arusha, Mbeya, Kigoma, Dodoma, Morogoro, Mtwara, Unguja na Pemba.

"Natambua mchango mkubwa wa maoni yaliyokwishatolewa hadi sasa kama Waziri wa nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji alivyoeleza. Nami nipende kutumia jukwaa hili pia kuzisisitiza Wizara zote, Taasisi za Umma, Idara zinazojitegemea,

"Wakala wa Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa, Sekta Binafsi, Watanzania wanaoishi Ughaibuni (Diaspora) na Wadau wote wa maendeleo kuendelea kutoa maoni pamoja na ushirikiano kwa timu Kuu ya Kitaalamu ya Dira pale mtakapohitajika kufanya hivyo."
Naye, Waziri wa Nchi - Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo amesema ameagiza maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kusisitiza ushirikishwaji wa wadau wote muhimu ndani na nje ya nchi ili kupata maoni kwa ustawi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Said Mtanda ameishukuru Serikali kwa kufanya kongamano hilo katika mkoa huo ili kukusanya maoni ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news