Kamishna Luoga asisitiza kasi,umakini na bidii kwa watumishi Wizara ya Nishati

DAR-Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amewataka Wataalam katika Wizara ya Nishati na taasisi zake kujikita katika kufanya kazi kwa kasi, umakini na bidii ili kuwafikishia wananchi nishati ya uhakika na kwamba hicho ndicho kiwe kipimo kikuu cha kutangaza kazi za wizara kwa wananchi.Kamishna Luoga amesema hayo wakati alipotembea Banda la Wizara ya Nishati na Taasisi zake katika Maonesho ya Kimataifa ya Biashara (SABASABA) yanayoendelea jijini Dar es Salaam.
“Sisi Wizara ya Nishati tumejipa changamoto ya kuongeza bidii zaidi ya kufanya kazi na kutoa huduma bora kwani Watanzania wanachotaka ni nishati ya kutosha ikiwemo ya umeme bila kuwa na usumbufu wowote.”

Ameeleza kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuhakikisha kuwa inatoa fedha za kutekeleza miradi ya uzalishaji, usafirishaji, usambazaji umeme pamoja na miradi mingine ya Nishati akitolea mfano mradi wa umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) unaotekelezwa kwa kiasi cha shilingi trilioni 6.5 ambao sasa umefikia asilimia 98.
Ametaja baadhi ya miradi mingine ya kimkakati inayoendelea kutekelezwa kuwa ni pamoja na ya usafirishaji umeme itakayounganisha Mkoa wa Katavi na Kigoma kwenye gridi ya Taifa ambayo ni mradi wa usafirishaji umeme kutoka Tabora hadi Katavi na Tabora hadi Kigoma pamoja na miradi ya kuboresha upatikanaji umeme katika mikoa ya Lindi na Mtwara.
Kuhusu Maonesho ya SABASABA amesema “nimetembelea mabanda ya Maonesho ya Wizara ya Nishati na Taasisi zake na kuona jinsi Wataalam wanavyohudumia wananchi kwa umahiri na kutoa huduma mbalimbali ikiwemo za kuunganisha umeme kupitia mfumo wa Nikonekt, kuonesha wananchi kwa vitendo matumizi ya nishati safi ya kupikia na kutatua changamoto mbalimbali ambazo wananchi wanaziwasilisha.”
Ameeleza kuwa, Maonesho hayo ni muhimu kwani Serikali inapata wasaa wa kutoa taarifa za utekelezaji wa majukumu yake kwa wananchi na pia kupata mrejesho wa huduma inazotoa, suala ambalo ni muhimu katika kupima utendaji kazi.
Kuhusu utekelezaji wa ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia, Mha. Luoga amewaasa wananchi kutumia nishati iliyosafi ambapo amewahamasisha kutumia majiko ya umeme yanayouzwa kwa gharama nafuu, yanatumia umeme kidogo na kupika chakula kwa muda mfupi ikiwa ni matokeo ya teknolojia mpya iliyobuniwa na TANESCO kwa kushirikiana na kampuni ya TaTEDO na SESCOM.
Aidha, amewataka wadau wa nishati hiyo kuhakikisha kuwa wanakuwa na kanzidata itakayojumuisha masuala mbalimbali ikiwemo idadi ya wananchi wanaotumia nishati iliyosafi, matumizi yake n.k ambayo itatumika kama moja ya njia za kujitathmini katika utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia na kuchukua hatua stahiki zitakazowezesha mkakati huo kutekelezwa kwa ufanisi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news