Rais Dkt.Samia aagiza Soko la Kariakoo likikamilika biashara iwe saa 24

ZANZIBAR-Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amemuagiza Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dkt. Selemani Jafo kuhakikisha kuwa biashara katika Soko la Kimataifa la Kariakoo zinafanyika saa 24 pindi ujenzi wa soko hilo utakapokamilika.
Mheshimiwa Rais Dkt.Samia ametoa agizo hilo leo Julai 5,2024 wakati wa hafla ya uapisho wa
viongozi wateule iliyofanyika Ikulu ndogo ya Tunguu jijini Zanzibar.
Aidha, Rais Dkt. Samia pia amemuagiza Waziri Dkt. Jafo afanye kazi kwa ukaribu na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Wizara ya Mipango na Uwekezaji pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ili kusimamia sekta ya biashara katika soko hilo.
Vile vile, Rais Dkt. Samia amemtaka Waziri Dkt. Jafo kuhakikisha kunakuwa na mahusiano mazuri baina ya wafanyabiashara na Serikali kote nchini pamoja na kutatua kero zao, hali itakayopelekea Serikali kukusanya mapato stahiki na wafanyabiashara kunufaika na biashara zao.
Katika kuhakikisha raia wa kigeni hawajihusishi na biashara zinazopaswa kufanywa na wazawa, Rais Dkt. Samia amemuelekeza Waziri Dkt. Jafo kufuatilia utoaji wa leseni kwa wazawa na wageni ikiwa ni pamoja na kusajili wafanyabiashara na kuwa na kanzi data yao.
Kwa upande mwingine, Rais Dkt.Samia amemtaka Kamishna Mkuu wa TRA, CPA Yusuph Juma Mwenda kuziba mianya ya ukwepaji kodi na kuongeza mapato ya ndani yatakayowezesha Serikali kutoa huduma kwa wananchi kupitia mapato hayo.
Rais Dkt.Samia pia amemuagiza Kamishna Mwenda kuhakikisha mifumo ya TEHAMA kati ya TRA na Mamlaka ya Bandari inasomana ili kuweza kukusanya kodi itakayosaidia kuwekeza katika miradi ya maendeleo.
Hali kadhalika, Rais Dkt. Samia amemuelekeza Kamishna Mwenda kuhakikisha wafanyabiashara wote nchini wanatumia Mashine za Kielektroniki (EFD) na kuwahamasisha wananchi kudai risiti kwa manunuzi wanayofanya.
Katika hafla hiyo, viongozi hao walioapa ni Waziri wa Viwanda na Biashara,Mhe. Dkt. Selemani Saidi Jafo (Mb),Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Dkt. Ashatu Kachwamba Kijaji ,Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Ismail Samamba na CPA Yusuph Juma Mwenda ambaye ni Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news