DAR-Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa, Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali itaendelea kutoa vibali vya ajira kwa kila mwaka katika Sekta ya Afya ili kupunguza changamoto ya uhaba wa watumishi kutokana na maendeleo katika sekta hiyo.
Rais Dkt. Samia amesema hayo leo Julai 31, 2024 wakati akifunga Kongamano la kumbukizi la Hayati Benjamin William Mkapa leo Julai 31, 2024 ambalo limewakutanisha wadau wa maendeleo katika Sekta ya Afya kutoka ndani na nje ya nchi wakijadili changamoto na namna ya kuzitatua katika upande wa rasilimali watu.
"Changamoto ya upungufu wa watumishi katika Sekta ya Afya inatokana na kukua kwa idadi ya watu ambapo inapelekea kuongezeka uhitaji wa wataalamu wa afya na walimu, lakini endapo Tanzania itakua kiuchumi changamoto hiyo itaondoka."

Aidha, Rais Samia amesema mafanikio katika Sekta ya Afya yanategemea na jitihada za pamoja ikiwemo Serikali, Sekta binafsi, Wadau, pamoja na Taaisi za kidini huku jukumu kubwa la Serikali ni kuweka vichocheo vya uwekezaji ili kuongeza ubora wa huduma za Afya nchini.
Kabla ya kufunga kongamano hilo, Rais Samia ameipongeza Taasisi ya Benjamin Mkapa Foundation kwa kujidhatiti kuboresha mifumo na nguvu kazi ya Afya kwa kuajiri watumishi wa mikataba huku baada ya mkataba kuisha wanaajiriwa na Serikali.