Rais Dkt.Samia awataka viongozi wawathamini na kuwaheshimu wananchi

DAR-Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewataka Viongozi kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia Ibara ya 8 (1) (a) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayowataka kuwathamini na kuwaheshimu wananchi.
Rais Dkt. Samia ameyasema hayo leo Ikulu, wakati akiwaapisha Viongozi mbalimbali wakiwemo Mawaziri, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu, Makatibu Tawala wa Mikoa pamoja na Balozi.
Aidha, Rais Dkt. Samia amewataka viongozi hao kusimamia viapo walivyoapa mbele ya Mamlaka iliyowateua na mbele ya wananchi wanaokwenda kuwatumikia kwa kuhakikisha maslahi ya wananchi yanalindwa.

Kwa upande mwingine, Rais Dkt. Samia amemuagiza Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Jerry Silaa kuendelea kusimamia kikamilifu uhuru wa habari kwa kushirikiana na wadau wa sekta hiyo.
Rais Dkt. Samia pia amemtaka Waziri huyo kusimamia kasi ya ujenzi wa minara ya mawasiliano simu vijijini na kuimarisha usikivu wa redio ya Taifa kwenye maeneo ya pembezoni.

Vile vile, Rais Dkt. Samia amemtaka Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mhe. Ridhiwani Kikwete kuhakikisha vijana wanapata ajira kupitia Wizara za kisekta kama vile kilimo, mifugo, uvuvi na madini.
Hali kadhalika, Rais Dkt. Samia amemtaka Waziri huyo kusimamia Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na kuhakikisha inaendeshwa kisayansi, inakuwa endelevu pamoja na kusimamia miradi inayotekelezwa na mifuko hiyo.
Kwa upande wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Rais Dkt. Samia amemtaka Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo kuboresha utendaji na kulinda heshima ya nchi kimataifa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news