Serikali yadahili wanafunzi 25,390 wa Afya

DAR-Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeongeza udahili wa wanafunzi wa Taaluma za Afya ngazi ya kati, kutoka wanafunzi 20,030 mwaka 2020 hadi kufikia wanafunzi 25,390 ili kupunguza changamoto za upatikanaji wa watumishi wa kada hiyo.
Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amesema hayo leo Julai 31, 2024 wakati akitaja maazimio ya mkutano wa siku tatu wa rasilimali watu ulioandaliwa na Taasisi ya Hayati Benjamin Mkapa ikiwa ni kumbukizi ya alioyafanya katika Sekta ya Afya kwenye Ukimbi wa Mikutano wa Kimataifa Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar aes Salaam.

"Wanafunzi waliodahiliwa katika vyuo vikuu ngazi ya Shahada walikuwa 5,674 mwaka 2023 ikilinganishwa na wanafunzi 4,324 mwaka 2020, hii itasaidia kupunguza changamoto ya upungufu wa watumishi inayopelekea wananchi kupata huduma kwa wakati."

Aidha, Waziri Ummy amesema kuwa Serikali imeongeza posho za madaktari anapoitwa nje ya saa za kazi, posho ya sare za wauguzi na ile ya kuchunguza maiti kuanzia mwaka wa fedha 2024/2025 ambayo wataiona ikiingia kwenye akaunti zao za benki.

"Tumeshaanza utekelezaji wa kuongeza 'OnCall allowance' za madaktari ambazo zilikuwa hazijaongezwa, posho ya sare ya wauguzi, posho ya kuchunguza maiti na nyingine kuanzia Julai hii na hili ulituelekeza Mhe. Rais."

Amesema, miongoni mwa mambo yaliyoibuka katika kongamano hilo ni uzalishaji wa madaktari, wauguzi, wafamasia, wataalamu wa maabara na kukosekana kwa ajira mambo ambayo Serikali imeahidi kuendelea kuyashughulikia.

"Katika kutatua changamoto hiyo tutakaa na mabaraza ya wanataaluma wakiwemo MAT, wafamasia, wauguzi, maabara ili tukubaliane njia bora ya kudhibiti watumishi wa Afya ambao wapo barabarani."

Waziri Ummy amesema miongoni mwa maazimio yaliyotokana na kongamano hilo ni pamoja na kuhakikisha hospitali zinaajiri watumishi wa mikataba na kwamba mchakato wa bima ya afya kwa wote utakapokamilika utaziwezesha na hospitali za chini kuajiri watumishi wa mikataba.

Ametaja maazimio mengine kuwa ni kuendelea kuwajengea uwezo wataalamu wa Afya, kuendeleza huduma za ubingwa na ubingwa bobezi kwa kuwasomesha wataalamu bingwa na bobezi kama ambavyo Serikali imeendela kuwasomesha kupitia mpango wa “Samia Health Super Specialization Program”.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news