MOROGORO-Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imetakiwa kuongeza uzalishaji na usambazaji wa mbegu za miche ya miti ili zifikie wananchi wengi zaidi na hatimaye kushiriki katika kuonkoa misitu iliyotoweka.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) wakati wa ziara ya kikazi katika Kituo cha Uzalishaji mbegu za Miti leo Julai 9,2024 mkoani Morogoro.
"Tuendelee kuongeza kasi ya ukusanyaji wa mbegu na vyanzo vya mbegu na pia tuongeze Bajeti kukiwezesha kituo hiki," Mheshimiwa Kairuki amesema.


Katika hatua nyingine Waziri Kairuki amewataka kutoa elimu kwa umma kupitia vyombo vya habari na wahariri ili jamii ifahamu umuhimu wa mbegu bora za miti.
"Ni lazima muwe na maabara ya kisasa na pia mkitangaze kituo hiki kijulikane tuna mbegu za miche aina gani na tuna maabara," ameongeza.


Kituo cha uzalishaji mbegu za Miti kiko chini ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania ambapo kinazalisha mbegu za miche ya matunda ya muda mfupi, miche ya mbao,kuni,kivuli, mapambo na miti ya kilimo mseto.