Waziri Simbachawene kubadilisha maisha ya wananchi wa Kibakwe kwa kuja na Mkakati wa Kilimo cha Umwagiliaji

DODOMA-Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Mbunge wa Kibakwe, Mhe. George Simbachawene amewataka wananchi wa Kibakwe kuendesha kilimo cha biashara kwa kutumia miundombinu ya umeme iliyopo huku akiwaahidi kuwaletea mradi mkubwa wa kimkakati wa umwagiliaji.
Mhe. Simbachawene ametoa kauli hiyo leo wakati akizungumza na wananchi kwa nyakati tofauti kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Idodoma na Malolo, Jimbo la Kibakwe, Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma ikiwa ni mwendelezo ziara yake ya kikazi katika jimbo hilo.
Mhe. Simbachawene amesema, kitendo cha umeme kufika katika vijiji hivyo kutaleta mapinduzi makubwa ambapo ni muda muafaka sasa wa kuhakikisha umeme huo unatumika kuendesha mashine ya kusukuma maji ya kumwagilia kwenye mashambani.
Amesema,awali changamoto kubwa ilikuwa ni kilimo cha umwagiliaji cha kutumia nishati ya dizeli na petroli ambapo ilikuwa ni ngumu kuona tija kutokana na gharama kubwa ya nishati hiyo.
Ameongeza kuwa, umwagiliaji umekuwa duni kutokana na mifereji inayotumika kuwa ni ya kizamani na inachangia upotevu mkubwa wa maji.

"Tunataka mabadiliko makubwa katika jimbo letu, tunatamani kuona umeme tulionao unatupeleka mashambani na sio kuutumia tu kwa ajili ya kuwashia taa pekee majumbani mwetu," amesema Mhe. Simbachawene.
Amesema,umeme huo utumike kusukuma maji ya kumwagilia usiku na mchana katika mashamba ya wananchi huku akisema miaka 10 ijayo anaviona vijiji hivyo vikiwa katika viwango vya juu kiuchumi.
Kwa upande wake Mkulima, Bwana Aidani Chihoma ametumia fursa hiyo kumshukuru Waziri Simbachawene kwa kupeleka umeme katika vijiji hivyo huku akisema ujio huo wa mradi huo wa umwagiliaji utasaidia kuona tija ya kilimo cha vitunguu na maharage.
Kijiji cha Idodoma na Malolo ni miongoni mwa vijiji katika Jimbo la Kibakwe vinavyosifika kwa kustawisha zaidi kilimo cha vitunguu na maharagwe ambapo uhitaji wa mazao hayo umekuwa mkubwa ndani na nje ya nchi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news