Afrika Kusini yawafukuza Walibya waliokamatwa kambi ya siri

JOHANNESBURG-Serikali ya Afrika Kusini imewafukuza raia 95 wa Libya ambao walikamatwa mwezi uliopita katika kambi ya siri inayodhaniwa ni ya kijeshi katika Jimbo la Kaskazini Mashariki mwa Mpumalanga nchini humo.
Picha na Zimlive.

Uamuzi huo umefikiwa Agosti 18,2024 ambapo Waziri wa Mambo ya Ndani wa Afrika Kusini, Leon Schreiber amesema, wizara yake itaendelea kutumia uwezo wake kuhakikisha sheria za uhamiaji zinaheshimiwa kote Afrika Kusini.

Inadaiwa raia hao wa Libya waliingia Afrika Kusini mwezi Aprili kwa vibali vya kusoma ili kuwa walinzi, na walikamatwa mwezi Julai, mwaka huu wakati wa msako wa polisi kwenye kambi ya mafunzo ya kijeshi katika mji wa White River huko Mpumalanga.

Kwa mujibu wa Jeshi la Afrika Kusini, vilipatikana vifaa vya mafunzo ya kijeshi na dawa za kulevya kwenye kambi hiyo.

Raia hao wa Libya wanadaiwa kupokea mafunzo ya kijeshi kinyume cha sheria, kukiuka masharti ya Visa zao na Sheria ya Uhamiaji nchini humo.(AP/NA).

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news