Balozi Nchimbi aitaka NIDA kuharakisha vitambulisho kwa wananchi wanaokidhi vigezo

KAGERA-Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi ameiagiza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, kuharakisha mchakato wa upatikanaji wa Vitambulisho vya Uraia (NIDA) kwa wananchi wa Ngara mkoani Kagera, wanaokidhi vigezo.
Nchimbi ameyasema hayo Agosti 7, 2024 alipokuwa akizungumza na maelfu ya wananchi wa Mji wa Ngara, katika Uwanja wa Posta, akiwa katika siku ya pili ya ziara yake mkoani Kagera, baada ya Mbunge wa Jimbo la Ngara Mhe. Ndaisaba George Ruhoro kuwasilisha kilio hicho kwenye mkutano huo.
Mapema pia kabla ya mkutano wa hadhara huo, Balozi Nchimbi alitoa maelekezo kuhusu suala hilo la upatikanaji wa vitambulisho vya NIDA, aliposimama kuwasalimia wananchi wa Kijiji cha Kumunazi alipokuwa njiani akitokea Biharamulo, kuelekea Ngara.

Akiwa ameambatana na wajumbe wa Sekretarieti ya CCM Taifa katika ziara hiyo; Ndugu Issa Haji Usi Gavu, Ndugu Amos Gabriel Makalla na Ndugu Rabia Hamid Abdallah, Balozi Nchimbi ameielekeza Wizara hiyo kuchukua hatua haraka ili changamoto hiyo imalizwe.
Amesema hata utaratibu wa kuruhusu watu kuazimana vitambulisho vya NIDA kwa shughuli mbalimbali ni jambo hatari, linaloweza kusababisha uhalifu.

"CCM itasimamia ili kuhakikisha suala hilo linafanyiwa kazi na kasi ya utoaji wa vitambulisho vya NIDA inapatikana," amesema Dk. Nchimbi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news