Kujiandikisha zaidi ya mara moja ni kosa Kisheria-INEC

MANYARA-Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi imesema kujiandikisha kuwa Mpiga Kura Zaidi ya mara moja ni kosa la kisheria kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 114(1) cha sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024.
Hayo yamesemwa na Mhe. Jaji Asina Omari, Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi na Jaji wa Mahakamu Kuu wakati akifungua Mkutano wa Tume na Wadau wa Uchaguzi katika Ukumbi wa Mikutano wa Mkuu wa Mkoa mkoani Manyara leo tarehe 25 Agosti, 2024.

“Nitoe rai kwenu, muwaelimishe wananchi wanaokwenda vituoni kwa ajili ya kuomba kuandikishwa kuwa wapiga kura, kuomba kuandikishwa kuwa wapiga kura ni mara moja tu ili kuepuka uvunjaji wa sheria,”amesema Mhe. Jaji Asina.
Mjumbe wa Tume, Mhe.Jaji Asina Omari amewapongeza wadau wa Uchaguzi na wananchi wa Manyara kwa kupata fursa ya mkoa wao kuwa katika mzunguko wa nne wa uboreshaji wa Daftari na kuwataka wawe mabalozi wazuri wa kusambaza taarifa na kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha na kuboresha taarifa ili zoezi hili lifanyike kwa ufanisi na mafanikio makubwa.

Mhe.Jaji Asina Omari aliwakumbusha Wadau wa Uchaguzi kuwa zoezi hili ni kwa mujibu wa Ibara ya 74(6) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 ikisomwa pamoja na Kifungu cha 16(5) cha sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 ambayo inatoa jukumu kwa Tume kusimamia na kuratibu uandikishaji wa wapika kura mara mbili kati ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge wa Jamhuri ya Muungano na Madiwani Tanzania Bara uliomalizika na kabla ya siku ya Uteuzi wa wagombea kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu unaofuata.
Aidha, mzunguko huu wa nne wa uboreshaji wa Daftari ia Kudumu la Wapiga Kura utajumuisha sehemu ya mkoa huu wa Manyara katika Halmashauri za Wilaya ya Babati, Babati Mji Hanang, na halmashauri ya Mbulu na mikoa ya Mara na Simiyu ambapo utaanza tarehe 04 hadi 10 Septemba, 2024 na vituo vitafunguliwa kuanzia saa 2:00 Asubuhi na kufungwa saa 12:00 kwa siku saba.

Hata hivyo, safari hii mfumo wa uandikishaji wapiga kura umeboreshwa ambapo kwa mara ya kwanza utamwezesha mpiga kura aliyemo kwenye Daftari kuanzisha mchakato wa kuboresha taarifa zake au kuhama kituo kwa kutumia aina zote za simu au Kompyuta.
Wapiga kura wanaotumia simu za kawaida (Maarufu kiswaswadu au kitochi) wanaweza kupiga namba *152*00# na kisha watabonyeza namba 9 na kisha wataendelea na hatua zingine kama itakavyoelekezwa kwenye simu husika.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news