Rais Dkt.Mwinyi aishukuru China kwa kuendelea kusaidia miradi ya maendeleo

ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi amesema, China imekuwa ikiisaidia Zanzibar katika mambo mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya hospitali.
Rais Dkt. Mwinyi amesifu ukarabati mkubwa wa Hospitali ya Abdalla Mzee Pemba, utoaji wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wafanyakazi wa sekta ya afya, msaada wa vifaa vya matibabu na dawa, pamoja na udhamini wa masomo kwa madaktari wazalendo.

Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi ameyasema hayo Agosti 26, 2024, Ikulu Zanzibar, alipozungumza na timu ya madaktari 29 kutoka kundi la 33, walioongozwa na Kaimu Balozi Mdogo wa China Zanzibar, Chang Ming, chini ya kiongozi wa madaktari hao, Dk. Yuzheng Huang, waliofika kumuaga baada ya kufanya kazi nchini kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Aidha, Dkt. Mwinyi ameishukuru Serikali ya China kwa ushirikiano wake na Zanzibar kupitia sekta mbalimbali za maendeleo, ikiwemo sekta ya afya, unaochangiwa na uhusiano wa kidiplomasia uliopo baina Zanzibar na China tangu kuasisiwa kwake.

Halikadhalika, Dk. Mwinyi amesema kuwa mbali na misaada hiyo, China pia imeisaidia Zanzibar kwa kutoa msaada wa kitaalamu katika udhibiti na kinga za maradhi mbalimbali, ikiwemo kichocho kwa Unguja na Pemba, pamoja na kuleta teknolojia mpya ya uchunguzi wa maradhi ya kansa.
Naye kiongozi wa timu ya madaktari hao, Dk. Yuzheng Huang, aliishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na uongozi wa Wizara ya Afya kwa ushirikiano waliowaonesha tangu walipofika Zanzibar mwezi Septemba mwaka 2023, pamoja na kusifia ukarimu wa watu wa Zanzibar.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news