Serikali itaendelea kutumia TEHAMA kukuza maendeleo-Dkt.Biteko

DAR-Serikali itaendelea kutoa kipaumbele katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano ili iweze kuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya kiuchumi kama inavyoelekezwa katika Dira ya Taifa ya 2025, Sera ya Maendeleo ya TEHAMA ya mwaka 2016 na Ilani ya CCM 2020-2025.
Hayo yamebainishwa leo Agosti 24, 2024 na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko wakati akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye uzinduzi wa mpango wa Ujuzi wa Kidigitali kwa wote (DigiTrack) uliowezeshwa na Huawei na Vodacom Foundation.

Amesema kuwa, Serikali inahamasisha matumizi ya TEHAMA ili kuwezesha wananchi hususani vijana na kizazi kijacho kushindana katika uchumi wa dunia.
"Kwa kuimarisha elimu ya TEHAMA, tunajenga jamii yenye ujuzi wa kutumia teknolojia kwa ufanisi, kubuni suluhisho za ubunifu, na kuchangia katika uchumi wa kidijitali. Hii itasaidia katika kuhakikisha kwamba maendeleo ya kidijitali yanakutanisha kila mmoja, bila kujali hali ya kiuchumi,"amesema Dkt. Biteko.
Ameongeza kuwa, Serikali inayoongozwa na Rais Samia itafanya kila linalowezekana kuhakikisha kwamba wawekezaji wanakuwa msaada katika kubadilisha hali maisha ya watu kupitia nyanja mbalimbali ikiwemo TEHAMA huku pia wawekezaji hao wakinufaika na uwekezaji wao.

Dkt. Biteko amesema uchumi wa kidijitali ni muhimu katika kuleta maendeleo kwa kuongeza ufanisi katika uzalishaji na na kuleta fursa na mapato ya ziada kwa wananchi.
Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Jerry Silaa amewapongeza Huawei na Vodacom kwa kuja na teknolojia ya Digi Truck ambayo inakwenda kuwa msaada kwa vijana wengi nchini ambayo itafika kila sehemu ili vijana wengi wajifunze.

Akizungumza katika hafla hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire amesema kwa kushirikiana na Huawei watapeleka huduma hiyo ya kidijitali katika kila pembe kwa watanzania kutoa elimu hiyo hususani kwa vijana ili kuwezesha kizazi cha kisses kinachoendana na mabadiliko ya kisayansi na kibunifu.
Teknolojia hiyo iliyozinduliwa leo kutoka kampuni ya Vodacom Tanzania na Huawei itawezesha wananchi kupata elimu na ujuzi wa TEHAMA.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali na wadau wa TEHAMA kutoka ndani na nje ya nchi ili kujionea uzinduzi huo muhimu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news