Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina yapokea gawio la shilingi bilioni 4.35 kutoka TAZAMA

DAR-Serikali ya Tanzania kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina imepokea Gawio la Shilingi Bilioni 4.35 kutoka Shirika linalosimamia Bomba la Mafuta kutoka Tanzania kwenda Zambia (TAZAMA).
TAZAMA imetoa gawio hilo baada ya kupita miaka mitano, mara ya mwisho ilitoa shilingi milioni 681.8 mwaka 2019.

Akizungumza katika hafla ya kupokea hundi ya Gawio hilo iliyofanyika leo Agosti 26,2024 jijini Dar es Salaam, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt.Doto Biteko amesema kitendo hicho ni hatua muhimu kwa Tanzania kwani mradi huo una miaka mingi na sasa matunda yanaonekana.
Amesema, Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan alipotembelea Zambia moja ya maelekezo yake ilikuwa ni miradi inayounganisha nchi hizo mbili isimamiwe vizuri ili ilete manufaa kwa nchi zote mbili na angefurahi kuona miradi kama Tazama inaleta si tu manufaa ya kikodi bali ichangie kunufaisha maisha ya watu.

“Mara ya mwisho kutoa gawio kwa serikali ilikuwa miaka mitano iliyopita, na sasa tumepokea fedha hizi, tunajivunia maana badala ya kuja na sababu na visingizio kadha wa kadha lakini mmekuja na fedha, kuna baadhi ya taasisi wanakuja na maneno mengi ya kijanja… unajua kulikuwa na Covid, tatizo la dola lakini nyie hamkuwa hivyo, tunatarajia wakati mwingine kutakuwa na habari njema zaidi,” alisema.

“Naipongeza bodi na uongozi wa Tazama kwanza kwa kufanya jambo hili liwezekane, nataka kuwahakikishia serikali yetu kupitia Wizara ya Nishati tuko kwenye mazungumzo mazuri ya kuongeza uwekezaji kwenye bomba letu la Tazama kama mnavyofahamu tunataka kupanua bomba lililopo kutoka nchi nane hadi 12 na litaanza muda si mrefu ili tusafirishe mafuta mengi kwenda Zambia na baadae kutoka Zambia kwenda nchi za Kongo (DRC) na majirani zetu."

Alisema pia wanakusudia kuanza ujenzi wa bomba jipya la inchi 24 na kwa sasa wapo kwenye hatua mbalimbali za manunuzi nia ni kuona mafuta mengi zaidi yanasafirishwa kwa bomba badala ya malori.
Kwa upande wake, Msajili wa Hazina Nehemiah Mchechu amesema Tazama sasa imeamka ikiwa na miaka takriban 58 tangu kuanzishwa kwake.“Umri huo kama mtumishi wa umma amebakiza miaka miwili kustaafu, anakuwa kidogo mnyonge mnyonge lakini kwa Tazama badala ya kuwa mnyonge ndio imekuja juu, imekuwa tofauti kidogo,” alisema.Amesema, mafanikio hayo ni moja ya faida za falsafa ya 4R za Rais Samia (Maridhiano, Ustahamilivu, Mageuzi na Ujenzi mpya.
Akizungumzia tukio hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Kitila Mkumbo alisema gawio hilo linadhihirisha jinsi ushirikiano wa nchi hizo mbili ulivyo imara.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news