Serikali yashauriwa kuanzisha Klabu za Mambo ya Fedha Shuleni

NA JOSEPHINE MAJULA

SERIKALI imeshauriwa kuwasimamia Wakuu wa Shule kuongeza kasi ya kuanzisha Klabu za mambo mbalimbali yakiwemo masuala ya fedha katika shule zilizopo nchini ili zitumike kutoa elimu hiyo pamoja na mambo ya kijamii.
Afisa Mchambuzi Hesabu Mwandamizi, kutoka Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana Bi. Mariam Omari Mtunguja, akitoa elimu kwa Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Kutwa Liwale, Bi. Shuweikha Barwany (kulia) na Bi. Zubeda Suphian baada ya kumalizika kwa semina ya utoaji elimu ya masuala ya fedha ambapo Timu ya Wataalamu ya Wizara ya Fedha ipo mkoani Lindi kutoa elimu hiyo.

Ushauri huo umetolewa na Mlezi wa Klabu katika Shule ya Sekondari ya Kutwa Liwale, Mwalimu Mustafa Ahmadi Likambako, alipokutana na Timu ya Wataalamu kutoka Wizara ya Fedha ambayo ipo mkoani Lindi kutoa elimu ya masuala ya fedha kwa makundi mbalimbali ya wananchi wakiwepo wanafunzi, wafanyabiashara, wakufunzi na wajasiriamali.
Kiongozi wa Wanafunzi Shule ya Sekondari ya Kutwa Liwale, Bw.Aktar Amir Issa, akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Wanafunzi wenzake baada ya kumalizika kwa semina ya utoaji elimu ya masuala ya fedha ambapo Timu ya Wataalamu ya Wizara ya Fedha ipo mkoani Lindi kutoa elimu hiyo.
Afisa Msimamizi Mkuu wa Fedha, Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha Bw. Salim Khalfan Kimaro, akizungumza na Wanafunzi na Wakufunzi wa Shule ya Sekondari ya Kutwa Liwale, wakati wa semina ya utoaji elimu ya fedha Wilaya ya Liwale mkoani Lindi ambapo mada mbalimbali zilifundishwa ikiwemo uwekezaji, mikopo na akiba.

“Katika shule yetu tuna Klabu tatu ya mazingira, masuala ya rushwa na femina, kwakuwa mimi ndio mlezi wa clubs hizi nimeona zinavyowasaidia wanafunzi kuwa na uelewa mpana wa masuala ya kijamii wanayojifunza muda wa ziada,”alisema Bw. Likambako.

Aliongeza kuwa upo uhitaji wa Wizara ya Fedha kuona umuhimu wa kuanzisha Klabu ya masuala ya fedha katika shule mbalimbali ili wanafunzi wafundishwe matumizi ya fedha tangu wakiwa wadogo ili wakiwa wakubwa wawe na uelewa wa masuala ya fedha.
Baadhi ya Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Kutwa Liwale, walioshiriki semina ya elimu ya fedha wakiangalia filamu yenye mada mbalimbali ikiwemo utunzaji wa akiba, uwekezaji, na nyinginezo iliyofanyika katika Ukumbi wa Shule hiyo Wilaya ya Liwale mkoani Lindi.

“Shuleni kwetu tuna matamasha mbalimbali huwa tunatumia jukwaa hilo kuwashindanisha wanafunzi wa Klabu mbalimbali na kutoa zawadi hii inasaidia kumfanya mwanafunzi awe makini darasani lakini kuwa na juhudi binafsi ya kusoma na kushika wanachofundishwa,” alisema Bw. Likambako.

Aliongeza kuwa zikianzishwa Klabu za masuala ya fedha katika shule itasaidia kupata mabalozi ambao ni wanafunzi na wakirudi nyumbani likizo wanakua walimu wazuri kwa wazazi wao na jamii inayowazunguka.

Naye Afisa Mchambuzi Hesabu Mwandamizi, kutoka Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana Bi. Mariam Omari Mtunguja, alisema kuwa wametoa elimu ya masuala ya fedha kwa makundi mbalimbali wakiwepo wanafunzi, wakufunzi, vikundi vya wajasiriamali na wafanyabiashara.

“Tumeona kiu ya wanafunzi kuuliza maswali mengi wakitaka kujua mitaji inatakiwa kuanzia shilingi ngapi, lakini waliuliza kama wanafunzi wanaruhusiwa kuwa wawekezaji nimeona kuna umuhimu wa elimu hii kuanza kutolewa mapema katika shule mbalimbali,”alisema Bi. Mtunguja.
Baadhi ya Wakufunzi wa Shule ya Sekondari ya Kutwa Liwale, walioshiriki semina ya elimu ya fedha wakiangalia filamu yenye mada mbalimbali ikiwemo utunzaji wa akiba, uwekezaji, maisha baada ya kustaafu, mikopo na nyinginezo iliyofanyika katika Ukumbi wa Shule hiyo Wilaya ya Liwale mkoani Lindi.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini WF, Lindi).

Kwa upande wake, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Liwale Day Bi. Zuleikha Hamidu, aliahidi kuanza kuweka akiba kwenye fedha za matumizi anazopewa na wazazi wake ili ziweze kumsaidia kwa baadae.

Timu ya Wataalamu kutoka Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Taasisi nyingine za Serikali ikiwemo Ofisi ya Rais- Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) na Tume ya Maendeleo ya Ushirika (TCDC), ipo mkoani Lindi kwa ajili ya kutoa elimu ya fedha kwa wananchi wa makundi mbalimbali ikiwemo wafanyabiashara, wanavikundi mbalimbali, wajasiriamali, wakufunzi na wanafunzi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news