Utafiti unaonesha asilimia 86.2 ya wanawake wanajihusisha na shughuli za madini-Dkt.Kiruswa

DODOMA-Matokeo ya utafiti mdogo uliofanywa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kwa kushirikiana na Chama cha Wachimbaji Wanawake Tanzania (TAWOMA) umeonesha zaidi ya asilimia 80 ya wanawake kutoka mikoa ya Shinyanga, Geita, Mara na Simiyu wanajishughulisha na shughuli za sekta ya Madini nchini.
Hayo yamesemwa leo Agosti 27, 2024 na Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa alipokuwa akijibu swali lililoulizwa na Mbunge wa Viti maalumu vya wanawake Fatma Hassan aliyetaka kujua idadi ya wanawake wanaomiliki migodi ya madini nchini.

Naibu Waziri amesema kuwa, shughuli za madini nchini zinafanyika katika maeneo mbalimbali kupitia watu binafsi na kampuni ambazo ndani yake kuna wanawake na wanaume.

Ameongeza kuwa, utafiti uliohusisha wanawake 992 umeonesha Wanawake 17 sawa na asilimia 1.7 wanamiliki migodi, wanawake 67 sawa na asilimia 6.8 wanamiliki maeneo ya uchimbaji (maduara) katika leseni za uchimbaji madini.

Vilevile, wanawake 855 sawa na asilimia 8.2 wanajishughulisha na kazi zinazohusiana na uchimbaji pamoja na uchenjuaji madini huku wanawake 53 sawa na asilimia 5.3 wanatoa huduma maeneo ya uchimbaji.

Dkt. Kiruswa ameongeza kuwa kulingana na umuhimu na mchango wanaotoa kwa taifa, Serikali itaendelea kuwasimamia na kuwapatia leseni wanawake wanaojishughulisha na uchimbaji wa madini ili kuongeza mchango wao kwenye sekta pia kuimarisha uchumi wao.

Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 ilibaini kuwa kuna takribani wanawake milioni 3 wanaoshiriki katika mnyororo mzima wa thamani madini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news