Young Africans Sports Club yatwaa Ngao ya Jamii 2024,Simba SC yaambulia nafasi ya tatu

NA GODFREY NNKO

MABINGWA wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Young Africans Sports Club (Yanga SC) ya jijini Dar es Salaam wametwaa Ubingwa wa Ngao ya Jamii 2024.
Ni baada ya kumenyana na Azam FC katika Dimba la Benjamin Mkapa lililopo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke jijini Dar Es Salaam leo Agosti 11,2024.
Kupitia fainali hiyo, Azam FC ilianza kuzifumania nyavu za Yanga SC baada ya Feisal Salum Abdalla (Fei Toto) kufunga bao la kwanza dakika ya 13 ya kipindi cha kwanza.

Bao hilo, lilionekana kuwatia hasira Yanga SC ndipo Prince Dube dakika ya 19 ya kipindi cha kwanza akasawazisha.
Dakika ya 28 ya kipindi cha kwanza, Yoro Diaby (OG) aliongeza bao la pili kwa Yanga SC ambalo lilidumu muda mfupi huku Stephanie Aziz Ki katika dakika ya 31 akaongeza lingine.

Kama walivyowahi kusema Waswahili kuwa, kutangulia si kufika hayo yalitimia kwa Azam FC ambao walitangulia kufunga, lakini hadi dakika 45 za kipindi cha kwanza kinatamatika, Yanga ilikuwa mbele kwa mabao 3-1.
Clement Mzize ndiye aliyezamisha jahazi la Azam FC dakika ya 90' baada ya kuzifumania tena nyavu zao ambapo hadi mtanange huo unaisha matokeo yalikuwa Yanga SC mabao 4 huku Azam FC wakiambulia moja.

Ushindi huo, unaiwezesha Yanga SC kutwaa ubingwa wa nane wa Ngao ya Jamii tangu michuano hiyo ilopoanza mwaka 2001 huku watani zao Simba SC wakiwa wameitwaa mara 10.

Simba SC vs Coastal Union

Awali katika mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu wa Ngao ya Jamii kati ya Simba dhidi ya Coastal Union uliopigwa hapo hapo Benjamin Mkapa umemalizika kwa Simba SC kupata ushindi wa bao moja.

Saleh Karabaka aliwapatia Simba bao hilo pekee dakika ya 11 baada ya kumalizia mpira wa krosi uliopigwa na Joshua Mutale.
Baada ya bao hilo, Simba SC waliendelea kuliandama lango la Coastal huku wakimiliki sehemu kubwa ya mchezo ingawa haaakuweza kutumia nafasi walizopata.

Kipindi cha pili Coastal walirudi kwa kasi na kufanya mashambulizi mengi langoni mwa Simba SC bila mafanikio.

Aidha,kiungo mkabaji Fabrice Ngoma alitolewa dakika ya 84 baada ya kuoneshwa kadi ya pili ya njano kufuatia kumchezea madhambi Mbaraka Yusuph wa Coastal Union.
Baada ya hatua hii sasa ni rasmi msimu mpya wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara (NBCPL) 2024/2025 umewadia.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news