BoT kuja na mwongozo wa kutatua malalamiko ya watumiaji wa huduma za fedha

DAR-Benki Kuu ya Tanzania (BoT) iko mbioni kuandaa mwongozo utakaoainisha utaratibu wa kufuatwa katika kutatua malalamiko ya watumiaji wa huduma za fedha.
Kaimu Mkurugenzi wa Ustawi na Huduma Jumuishi za Fedha, Bw. Sadiki Nyanzowa, amesema mwongozo huo unalenga kuongeza ufanisi wa kushughulikia malalamiko hayo pamoja na kuleta usawa wa namna ya kushughulikia malalamiko kwa watoa huduma za fedha wote nchini.
Alikuwa akizungumza na wawakilishi kutoka mabenki walioshiriki katika warsha ya utatuzi wa malalamiko ya watumiaji wa huduma za fedha nchini iliyofanyika BoT jijini Dar es Salaam.
Bw. Nyanzowa amesema mapendekezo na maoni mbalimbali yaliyotolewa katika warsha hiyo yataisaidia BoT kutengeneza mwongozo utakaohakikisha malalamiko ya watumiaji wa huduma hizo yanashughulikiwa na kutatuliwa kwa ufanisi.

“Maoni na mapendekezo yaliyotolewa katika warsha hii yatakuwa ni sehemu muhimu katika mwongozo utakaotengenezwa na Benki Kuu ambao una lengo la kuboresha mchakato wa kutatua malalamiko ya watumiaji wa huduma za fedha kwa ajili ya kuongeza imani ya watumiaji wa huduma hizo,” amesema.
Aidha, ameziasa benki kuendelea kuimarisha michakato na taratibu za ndani za kutatua malalamiko ya watumiaji wa huduma za fedha huku zikihakikishi taratibu hizo zinaendana na miongozo mbalimbali inayotolewa na BoT.

“Huku BoT ikiendelea kutoa miongozo mbalimbali ya kushughulikia malalamiko ya watumiaji wa huduma za fedha, ni muhimu kwa taasisi zinazotoa huduma hizo kuzingatia miongozo hiyo,” amesema.
Pia, amesema watoa huduma za fedha wanaweza kutumia malalamiko hayo kama fursa ya kuboresha huduma na bidhaa zao na hatimaye kuleta utulivu katika sekta ya fedha.

“Kwa kutazama malalamiko kuwa ni fursa ya kuboresha na kukua, badala ya kuwa ni kikwazo, watoa huduma za fedha wanaweza kupunguza vihatarishi, kujenga imani pamoja na kuleta utulivu katika sekta ya fedha kiujumla,” Bw. Nyanzowa amesema.
Nao washiriki wa warsha hiyo, wameishukuru na kuipongeza Benki Kuu kwa kupokea maoni na mapendekezo mbalimbali kutoka kwao ambayo yatatumika katika kutengeneza mwongozo wa kutatua malalamiko ya watumiaji wa huduma za fedha.

Warsha hiyo, inayofanyika katika ofisi za BoT Dar es Salaam inatarajia kufikia tamati tarehe 20 Septemba, 2024, kwa ushiriki wa watoa huduma za fedha wasiokuwa mabenki.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news