KILIMANJARO-Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Kilimanjaro,Patrick Boisafi akiwa ameambatana na wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa wametembelea mradi wa Maabara ya Kisasa ya Kupima Ubora wa Maji ambao umetekelezwa na wataalamu wa ndani kutoka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Moshi (MUWSA).
Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo mbele ya kamati hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa mamlaka hiyo, Mhandisi Kija Limbe amesema, kiasi cha shilingi 81,859,500 zimetumika kwa ajili ya ujenzi pamoja na ununuzi wa baadhi ya vifaa vya maabara hiyo.
Mhandisi Limbe ameeleza pia mradi huu umetumia mapato ya ndani ya mamlaka hiyo na mradi huo umekamilika kwa asilimia 100.
Aidha, kamati hiyo imeweka wazi kuridhishwa na utekelezaji wa mradi huo ambao thamani ya fedha zilizotumika zinaonekana.

Ujenzi wa maabara hiyo ya kisasa unalenga kuendelea kuwahakikishia wananchi usalama wa maji wanayokunywa kutoka bombani.