Profesa Mushi afungua mafunzo ya MAED chini ya TAEC

ARUSHA-Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Profesa Daniel Mushi leo Septemba 10, 2024 afungua rasmi kozi ya Kikanda ya mafunzo kuhusu Uchambuzi wa Mahitaji ya Nishati kulingana na utumiaji wa Muundo wa Uchambuzi wa Mahitaji ya Nishati wa IAEA (MAED).
Mafunzo haya yaliyoanza rasmi jana tarehe 09 Septemba 2024 katika hoteli ya Corridor Spring jijini Arusha yanaratibiwa na Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) kwa kushirikiana na Shirika la Nguvu za Atomu Duniani (IAEA) na Shirika la Umeme la Afrika Mashariki (EAPP).
Kozi ya mafunzo inalenga kuongeza uwezo wa mahitaji ya nishati kwa wanasayansi, wapangaji mipango na watoa maamuzi katika nchi za ukanda wa nishati wa Afrika Mashariki.
Malengo makuu ni kuwapa ufahamu na kuwawezesha washiriki matumizi ya MAED kwa uchanganuzi wa mahitaji ya nishati, kusaidia mikakati ya nishati ya kitaifa na kikanda kwa maendeleo endelevu ya nishati na kuwezesha maamuzi yanayotokana na data katika sera ya nishati na ugawaji wa rasilimali.

Mafunzo yamejumuisha washiriki 50 kutoka nchi wanachama wa EAPP ambazo ni: Misri, Sudan, Sudan Kusini, Djibouti, Somalia, Ethiopia, Uganda, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Kenya, Burundi, Rwanda na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mafunzo haya yatawapa washiriki ujuzi wa vitendo katika utabiri na uchambuzi wa mahitaji ya nishati kwa kutumia zana ya MAED. Mazingatio zaidi yamelenga katika kuchanganua mahitaji ya nishati kwa kusisitiza upangaji na sera za nishati, mambo ya kiuchumi ya kijamii yanayoathiri mahitaji ya nishati kwa kutabiri mahitaji ya nishati ya siku zijazo.
Kozi hiyo itaendeshwa kwa wiki mbili ikijumuisha mafunzo ya vitendo, masomo ya kifani, na mazoezi shirikishi ili kuhakikisha kuwa washiriki wanaweza kutumia maarifa na ujuzi waliopata kwenye matukio ya ulimwengu halisi katika nchi zao. Mafunzo hayo yatafungwa Ijumaa, tarehe 20 Septemba, 2024.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news