ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi ameihakikishia Uingereza kwamba Zanzibar inaendelea na mikakati na juhudi kubwa ya kuhakikisha inadhibiti na kuumaliza ugonjwa wa trakoma hapa nchini.

Rais Dkt. Mwinyi amesema hatua iliyofikiwa na Zanzibar ya kukabiliana na magonjwa mbalimbali inatokana na juhudi kubwa na misaada ya Afya inayotolewa na Uingereza na kumuahidi kuwa Zanzibar itaendelea kufanyakazi kwa juhudi zaidi ili kupambana na magonjwa hasa yasiyoambukiza (NCDs) yanayoathiri ustawi wa jamii.
Pia, Rais Dkt. Mwinyi alieleza kufarajika kwake kwa misaada ya mafunzo ya kitaalamu ya kuwajengea uwezo wafanyakazi wa Sekta ya Afya hasa katika kukabiliana na maradhi yasiyoambukiza yanayotolewa na nchi hiyo ambayo yamekuwa kichocheo muhimu cha kuleta mafanikio kwenye sekta ya Afya na kusisitiza misaada hiyo kuendelezwa.
Dkt. Mwinyi alimuhakikishia Princess Sophie kuwa Zanzibar inaendelea kuweka mkazo zaidi na kuhakikisha huduma bora za sekta ya Afya hususan kuimarisha huduma za kitengo cha uzazi kwa mama na mtoto na kuwataka wafadhili na washirika wengine wa Maendeleo kuendelea kuiunga mkono Zanzibar.



Princess Sophie (Duchess of Edinburgh) ni Mke wa mtoto wa mwisho wa aliyekua Malkia wa Uingereza, Elizabeth II, Prince Eduward ambaye ni mdogo wa Mfalme wa sasa wa Uingereza, Charles III.