Serikali yadhamiria mageuzi makubwa kilimo cha umwagiliaji nchini

RUVUMA-Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema,Serikali imejipanga kuinua Sekta ya Umwagiliaji kwa asilimia 50 ifikapo 2030.
“Serikali imewekeza katika sekta ya umwagiliaji, na ifikapo 2030, kilimo cha umwagiliaji kinatarajiwa kufikia asilimia 50 ya kilimo nchini,”amesema Rais Dkt. Samia.

Rais Dkt.Samia amesema hayo wakati akihutubia wananchi katika Viwanja vya Majimaji mkoani Ruvuma, ambapo amezungumza na wananchi kuhusu ziara yake hiyo mkoani humo, na kueleza mafanikio, mipango na maagizo mbalimbali ya serikali.

Amesema, alikagua ununuzi wa mahindi katika maghala ya NFRA na kuweka jiwe la msingi kwa ujenzi wa maghala 28 yenye uwezo wa kuhifadhi tani 28,000 za mazao ya nafaka, kisha alitembelea shamba la kahawa la Aviv na kusisitiza umuhimu wa kilimo cha kahawa.

Rais Samia ameongeza kuwa Serikali imetoa ruzuku ya mbolea yenye thamani ya bilioni 83.5, huku matumizi ya mbolea yakiongezeka kutoka tani 32,139 mwaka 2022 hadi tani 123,049 mwaka 2023, ambalo ni sawa na ongezeko la 283%.

Kwa upande wa zao la korosho, uzalishaji umeongezeka kutoka tani 15,000 hadi tani 29,109 kwa msimu wa 2023/2024, na lengo ni kufikia tani 55,730 msimu wa 2024/2025. Serikali pia imeandaa miche bora ya kahawa milioni 20 na kuigawa kwa wakulima bure, ikilenga kuboresha masoko ya kimataifa.

“Uzalishaji wa tumbaku umeongezeka kutoka tani 250 mwaka 2021 hadi tani 4,100 msimu wa 2023/2024”, amesema Rais Samia

Rais Dkt.Samia ameongeza kuwa Mkoa wa Ruvuma una miradi 33 ya umwagiliaji yenye thamani ya shilingi bilioni 32.4.

Kupitia NFRA, serikali imeunda mifumo ya kununua tani 170,000 za nafaka kwa thamani ya shilingi bilioni 119. Hadi sasa, tani 63,467 zimenunuliwa kwa thamani ya shilingi bilioni 44.43. Serikali itaendelea kujenga uwezo wa NFRA ili kuhakikisha usalama wa chakula nchini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news