Sitavumilia udanganyifu-Mwenyekiti wa Bodi ya NHIF

ARUSHA-Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Bw. Eliud Sanga amewaonya watumishi, watoa huduma, waajiri na wanachama wanaojihusisha na vitendo vya udanganyifu kuacha mara moja kwa kuwa bodi yake haitavumilia hilo.
Ametoa onyo hilo Septemba 12,2024 wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi la NHIF jijini Arusha.

“Kwa watumishi wa mfuko, wanachama na watoa huduma wasio waaminifu wanaojihusisha na udanganyifu waache mara moja, hatuna uvumilivu katika kuona yeyote akijinufaisha kupitia huduma zinazotolewa tunahitaji kuona mfuko ukiwa hai na ukitoa huduma nzuri,” amesisitiza.

Aidha, ameitaka Menejimenti kuhakikisha inaimarisha mifumo yake ya ndani ili iweze kubana mianya yote ya udanganyifu na iwezeshe utoaji wa huduma bora na kwa wakati.
Akizungumzia utendaji kazi wa watumishi, amewataka kujipima wenyewe na kuhakikisha wanafanya kazi kwa bidii, weledi na kwa kuzingatia maadili na taratibu zote zilizopo na kuachana na tabia za kuweka makundi mahala pa kazi.

“Tusitengeneze makundi ndani ya mfuko wetu, tengenezeni mfumo mzuri wa utendaji kazi ili muweze kutoa huduma bora kwa wadau wetu na matarajio ya Serikali yaweze kufikiwa,” amesema Mwenyekiti wa Bodi NHIF.
Alitumia fursa hiyo kumpongeza Mkurugenzi Mkuu Dkt. Irene Isaka kwa kuaminiwa na Serikali kuiongoza NHIF ambayo ni taasisi nyeti yenye dhamana ya utoaji wa huduma za matibabu.

Amewataka watumishi kumpa ushirikiano na kumtumia vizuri katika uboreshaji wa huduma kwa kuwa anao utaalam wa kutosha katika eneo la hifadhi ya jamii.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu,Dkt. Isaka, amemuahidi Mwenyekiti wa Bodi kuwa atasimamia Mfuko kwa weledi na uaminifu mkubwa.

“Naomba kuweka wazi kwamba sina uvumilivu (zero tolerance) kwenye masuala ya udanganyifu na uzembe nitasimamia kuhakikisha tunaongeza wigo wa wanachama, tunatoa huduma bora kwa wanachama wetu. Nitasimamia matumizi ya TEHAMA, tumeanzakubana matumizi ili tupunguze nakisi ya Mfuko.
"Pia tumedhamiria kuboresha mahusiano yetu na watoa huduma na wanachama wetu. Hivyo, tutafanya upekuzi kwa watumishi wote na tutatoa mafunzo ya ndani (huduma kwa wateja, usajili, uchakataji madai, kupinga udanganyifu, matumizi ya mifumo, ununuzi na uwekezaji) kwa lengo la kuleta ufanisi," amesema Dkt. Isaka.

Akizungumzia maandalizi ya utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, amesema Mfuko umeanza matayarisho hasa katika eneo la utoaji wa elimu kwa umma, mifumo itakayotumika katika kuandikisha wanachama, kukusanya michango na kuchakata madai.“Tumeweka mipango yetu vizuri katika kutekeleza hili la bima ya afya kwa wote, tunajua matarajio ya Serikali katika jambo hili, hivyo nikuahidi kuwa tutafanya kazi kwa kujituma ili kufanikisha azma ya serikali," amesema Dkt. Isaka.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news