Huu wosia wa baba

NA LWAGA MWAMBANDE

LEO Oktoba 14 Watanzania tunaadhimisha miaka 25 ya kumbukizi ya kifo cha Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. 

Ni miaka 25 ambayo ilitanguliwa na miaka zaidi ya 70 ya uhai wake ambapo muda mwingi aliutumia kulitetea na kulipigania Taifa la Tanzania.

Miongoni mwa mambo muhimu kwa Hayati Baba wa Taifa wakati wa uhai wake ilikuwa ni kujitolea kwa ajili ya taifa katika maisha yake yote huku akionesha uzalendo wa hali ya juu.

Ukirejea katika hotuba za Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere hususani ile ya mwaka 1958 pale Jangwani jijini Dar es Salaam ambayo iliamsha vuguvugu la kudai Uhuru, utaona dhairi kuwa Mwalimu Nyerere alikuwa mzalendo wa kweli.

Kwa pamoja turejee sehemu ya hotuba ile ya Jangawani kama alivyobainisha Hayati Baba wa Taifa..."Tunajua elimu ni kitu kikubwa sana na ndiyo tunayoitaka.

...lakini wanatuambia eti Muingereza ndiye atakayetupa elimu hiyo, sasa ngoja niwaulizeni. Na watu wenye magazeti ninawaulizeni sasa jambo kubwa.

"Eti, Muingereza ndiye atakayetupa elimu ile ya kutuwezesha nchi yetu, sasa ngoja niwaulize jambo moja, sijui watu wangapi, umati uliopo hapa, ninawaombeni pole pole ndugu zangu..ninawaombeni pole pole, Waingereza wamekaa Tanganyika miaka 40.

"Wengi wetu hapa tumezaliwa chini ya utawala wa Uingereza na hawa wanaotutawala watu wengi wamezaliwa katika muda ule ule, ninawaombeni ndugu zangu bila kuona haya hata kidogo...hata kidogo.

"Watu mlio katika umati huu msione haya hata kidogo, mliosoma mpaka darasa la 10 nyoosheni mkono, msione haya watu wote ambao mmesoma mpaka darasa la 10 katika umati huu nyoosheni mikono msione haya.

"Msione haya nyoosheni mikono, watu waliosoma mpaka darasa la 10 Kizungu nyoosheni mikono na watu wa magazeti simameni muwahesabu ninyi wenyewe. Watu waliosoma mpaka darasa la 10 Kizungu nyoosheni mikono, kazi ya Muingereza aliyoifanya miaka 40 itazameni wote hapa.

"Itazameni kazi ya Muingereza, kazi aliyoifanya katika nchi hii miaka 40, nyoosheni mikono jamaa wawaone, kina mama ninyi mmesema mmesoma mpaka darasa la 10, nyoosheni mikono, waoneni na wala sisemi kama vile ninawatanieni.

"Nyoosheni watu wa magazeti waione mikono ya umati wote huu waliosomeshwa na Muingereza katika muda wa miaka 40 mpaka darasa la 10, mnaiona mikono yenyewe tunaweza kuihesabu wakifika 200 ni bahati.

...wakifika 200 bahati, kazi ya Muingereza aliyoifanya kwa miaka 40 kwa Dar es Salaam, siyo... Dar es Salaam ni ya watu wenye elimu kubwa sana, miaka 40 teremsheni mikono yenu, nyoosheni mikono watu ambao mmesoma mpaka darasa la 12 kazi ya Muingereza miaka 40. Ebu nyoosheni...
Kutokana na upendo wa Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere kwa Tanzania, wakati akiendelea na matibabu huko jijini London, Mama Maria Nyerere amewahi kunukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari akieleza kuwa, alimuachia ujumbe muhimu ambao ni...

"Najua nitakufa, sitapona ugonjwa huu, nawaacha Watanzania wangu. Najua watalia sana. Nami nitawaombea kwa Mungu.

"Ninaondoka nikiwa nimewaachia Taifa moja lenye umoja na amani. Wosia wangu kwao waipende nchi yao kama wanavyowapenda mama zao. Wajue hawana nchi nyingine zaidi ya Tanzania." 

Aidha, kwa wosia huo, mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasisitiza kuwa kila Mtanzania anapaswa kuwa mzalendo namba moja kwa Taifa la Tanzania na kuhakikisha anadumisha amani, upendo na mshikamano. Endelea;

1. Vile wampenda mama, vivyo hivyo penda nchi,
Si mimi ninayesema, alisema mwenye nchi,
Yeye alishika tama, huku aiaga nchi,
Huu wosia wa baba, Mwalimu J. Nyerere.

2. Huu wosia wa baba, Mwalimu J. Nyerere,
Siku zipokuwa haba, kifo kikiwa ni sare,
Alituusia baba, hiyo hekima ya bure,
Vipi waipenda nchi, ndivyo wampenda mama?

3. Vipi waipenda nchi, ndivyo wampenda mama?
Wewe ndiye mwananchi, nchi aliacha njema,
Umekaa kwenye kochi, nchi bora kama mama?
Aliyosema Nyerere, hebu rudia rudia.

4. Aliyosema Nyerere, hebu rudia rudia,
Wala usiseme sore, nchi ukiibia,
Ni bora uone gere, kunyonya ukiachia,
Mama aweza toweka, nchi iko pale pale.

5. Mama aweza toweka, nchi iko pale pale,
Yuko hai furahika, nchi bado iko pale,
Amekufa sikitika, nchi iko pale pale,
Nchi unapoipenda, pendo lizidi la mama.

6. Nchi unayoipenda, pendo lizidi la mama,
Kinamama wanakwenda, wanatuachia homa,
Na kinababa waenda, tunabakia yatima,
Nyerere lishaondoka, bado ipo Tanzania.

7. Nyerere lishaondoka, bado ipo Tanzania,
Hii haitatoweka, hadi mwisho wa dunia,
Sisi tutabadilika, wengine watasalia,
Tuipende nchi yangu, kama kupenda wazazi.

8. Tuipende nchi yetu, kama kupenda wazazi,
Hapo tutakuwa watu, kama tunachapa kazi,
Yoyote yaliyo butu, tusifanye kwetu dozi,
Tanzania Tanzania, tuipende nchi yetu.

9. Tanzania Tanzania, tuipende nchi yetu,
Tufanye mambo kwa nia, tusiharibu misitu,
Kodi kutoilipia, tusiendekeze katu,
Alituasa Mwalimu, watuasa viongozi.

10. Alituasa Mwalimu, watuasa viongozi,
Hayo maonyo adhimu, vema kufanyia kazi,
Tanzania itadumu, uchumi kipanda ngazi,
Ya kale kweli dhahabu, twajifunza kwa Nyerere.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news