Kamati za Bunge kuanza Oktoba 7 hadi 25,2024

DODOMA-Shughuli za Kamati za Kudumu za Bunge kwa mwezi Oktoba, 2024 zitaanza tarehe 7 hadi tarehe 25 Oktoba, 2024. Shughuli hizo ni pamoja na vikao vya Kamati kwa ajili ya maandalizi ya Mkutano wa Kumi na Saba wa Bunge unaotarajiwa kuanza siku ya Jumanne tarehe 29 Oktoba, 2024.
Katika kipindi hicho, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) zitatangulia kuanza vikao tarehe 7 Oktoba, 2024. 

Kamati zilizosalia zitaanza vikao tarehe 15 Oktoba, 2024. Vikao vya Kamati zote vitafanyika Dodoma na vitaendelea hadi tarehe 25 Oktoba, 2024. Shughuli zitakazotekelezwa wakati wa Vikao vya Kamati za Bunge katika kipindi hicho ni kama ifuatavyo:-

Kuchambua Miswada ya Sheria

Shughuli hii itatekelezwa na Kamati tatu (3) za Bunge ambazo ni Kamati ya Miundombinu, Kamati ya Utawala, Katiba na Sheria na Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma.

Kuchambua Sheria Ndogo

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo, itafanya Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni katika Mkutano wa Kumi na Sita.

Kupokea Taarifa za Utendaji wa Serikali na Taasisi zake

Kamati kumi na moja (11) za kisekta zitapokea na kujadili taarifa mbalimbali za utendaji wa Serikali na Taasisi zake. Aidha, Kamati ya Bajeti itapokea taarifa mbalimbali kutoka Serikalini kwa lengo la kufuatilia utekelezaji wa shughuli za Wizara ya Fedha na masuala yanayohusu vyanzo vya mapato ya Serikali.

Kuchambua Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali

Kamati mbili (2) zinazosimamia matumizi ya fedha za umma, zitachambua Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusu Hesabu za Wizara, Mashirika ya Umma na Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa kwa Mwaka wa Fedha unaoishia tarehe 30 Juni, 2023.

Matokeo ya uchambuzi huo yanatarajiwa kuwasilishwa Bungeni na kujadiliwa wakati wa Mkutano wa Kumi na Saba wa Bunge utakaoanza tarehe 29 Oktoba, 2024.

Kuchambua Taarifa za Uwekezaji wa Mitaji ya Umma

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) itapokea na kuchambua taarifa za uwekezaji wa mitaji ya umma ili kubaini iwapo uwekezaji huo una ufanisi na kwamba, umezingatia taratibu na miongozo mujarabu ya biashara.

Ratiba ya Shughuli za Kamati inapatikana katika tovuti ya Bunge ambayo ni www.bunge.go.tz

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news