Mheshimiwa Pinda,SEOM wakutana na Machifu wa Botswana

GABORONE-Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC-SEOM), Mhe. Mizengo Pinda na ujumbe wake wa SEOM wamekutana na kuzungumza na machifu kutoka koo mbalimbali za nchini Botswana katika kikao kilichofanyika jijini Gaborone tarehe 27 Oktoba 2024 ikiwa ni sehemu ya vikao ambavyo SEOM imekuwa ikifanya na wadau mbalimbali wa uchaguzi nchini humo.
Mhe. Pinda ametumia kikao hicho kuwajulisha machifu hao kuhusiana na kazi ya uangalizi wa uchaguzi mkuu wa Botswana kuanzia maandalizi, mwenendo wake na jinsi mambo yalivyo wakati huu wa uchaguzi ikiwa ni kutekeleza jukumu la Uangalizi kwa kuzingatia misingi na miongozo ya uchaguzi wa kidemokrasia iliyowekwa na SADC.
Aliwaambia machifu hao kuwa SEOM imekuwa ikikutana na wadau mbalimbali na kuzungumza nao moja kwa moja na hivyo kupata picha halisi ya jinsi mwenendo na maandalizi ya uchaguzi huo yalivyo na kuongeza kuwa SEOM imepeleka waangalizi wake katika majimbo yote ya uchaguzi ili kuangalia hali inavyokwenda, itakavyokuwa siku ya uchaguzi na baada ya uchaguzi.
Akizungumza katika kikao hicho Kiongozi wa Machifu wa Botswana Chief Gaborone toka kabila la Batlokwa alisema wao kama machifu wana jukumu la kuhakikisha koo zao hazigawanyiki licha ya kuwa wananchi wao ni wafuasi wa vyama vya siasa na kwa kufanya hivyo amani na usalama vitaendelea kuwepo katika maeneo yao.

Alisema wao wakiwa viongozi wa kimila na kijadi nchini humo wana wajibu wa kuwahimiza wananchi kushiriki katika michakato ya siasa ili waweze kuchagua viongozi wa kisiasa ambao wataongoza nchi kwa kipindi husika.
Amesema wao sio wanasiasa ila wanashirikiana na viongozi serikali kuhakikisha wananchi wanashiriki kikamilifu katika shughuli za siasa kwa kufuata sheria, kanuni, taratibu na miongozo iliyopo akitolea mfano wa Tume Huru ya Uchaguzi ya Botswana ilivyowafuata na kuwajulisha juu ya juu ya kufanyika kwa zoezi la uandikishaji wapiga kura na kuwaomba kuwasaidia kufikisha ujumbe huo wa uandikishaji wapiga kura kwa wananchi kwenye maeneo yao.

Naye Chifu Lotlamoreng kutoka kabila la Barolong amesema kama chifu akitaka kujihusisha moja kwa moja na masuala ya siasa ni lazima aondoke katika kazi ya uchifu ili aweze kuwa huru kujihussiha na masuala ya siasa nchini humo.
Wamesema machifu hawajazuiwa kugombea nafasi za siasa ila wanatakiwa wajue kuwa ukiamua kugombea na kushiriki kama mgombea unatakiwa kuondoka katika ofisi ya chifu ili kuepuka mgogoro wa maslahi na sheria Sheria ya Machifu ya mwaka 2008 ambayo inawatambua machifu na ofisi zao nchini Botswana.

Ameongeza kuwa, katiba ya Botswana pia inatambua Ofisi ya Machifu na inawatambua machifu hao ambo wako zaidi ya 500 wakiwamo machifu wanawake ambao wanakaribia 100.
Katika mkutano mwingine, SEOM ilikutana na Kiongozi wa wa Chama cha Real Alternative, Bw. Gaontebale Mokgosi ambaye alionyesha wasiwasi kuhusu maandalizi ya uchaguzi huo ambayo yamefanywa na Tume Huru ya Uchaguzi (IEC), akitaja kuchelewa kwa uchapishaji wa karatasi za kupigia kura kama mfano wa mandalizi duni ya uchaguzi huo na wanadhani kuwa IEC haiko tayari kuendesha uchaguzi huru na wa na haki.

Chama hicho kilisisitiza umuhimu wa kuongeza utoaji wa elimu ya wapiga kura na kupendekeza kuwa IEC inapaswa kushirikiana kwa karibu na vyama vya siasa nchini Botswana ili kuhamasisha watu wengi zaidi kushiriki zoezi la kuandikisha wapiga kura na kujitokeza kupiga kura.

Pia walisisitiza umuhimu wa ofisi ya ushirikiano wa vyama vya kisiasa kutakiwa kufanya kazi zaidi mwaka huu wa uchaguzi kinyume na ilivyokuwa kwakuwa ofisi hiyo ina jukumu muhimu la kuunganisha IEC, vyama vya kisiasa, na raia kwa ujumla.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news