Serikali kuchukua hatua kwa watumishi wa umma wanaokiuka maadili

NA LUSUNGU HELELA
Dodoma

SERIKALI imesema itaendelea kuchukua hatua dhidi ya watumishi wa umma wanaothibitika kukiuka maadili ya utumishi wa umma huku ikiahidi kuwekeza zaidi katika matumizi ya TEHAMA ili kudhibiti vitendo vya ukiukwaji wa Maadili. Katibu Mkuu, UTUMISHI, Bw.Juma Mkomi ametoa kauli hiyo leo jijini Dodoma wakati akifunga Kikao kazi cha kubadilishana uzoefu wa masuala ya Maadili na Utawala Bora baina ya Taasisi Simamizi za Maadili ya Utendaji na Mamlaka Simamizi za Maadili ya Kitaaluma.

Amesema,Serikali haitawafumbia macho watumishi wala rushwa na walevi na wenye tabia na mienendo isiyofaa kwenye jamii.
‘’Hivi karibuni nimewahamisha watumishi wanne kutoka wizara fulani wanaotuhumiwa kushiriki mapenzi ya jinsia moja na kuna baadhi ya watumishi wanalala baa na asubuhi wanakwenda kazini wakiwa wachovu na hawajapiga mswaki na hivyo kuwapa shida wananchi wanapowahudumia,’’ ameng’aka Katibu Mkuu Mkomi.

Amesema, dhana ya utumishi wa umma ni maadili na bila maadili hakuna utumishi wa umma hivyo Serikali itaendelea kufanya tahtmini kwa kina kuhusu tabia na mienendo ya watumishi wa umma wakati wote.
Kufuatia hatua hiyo, Mkomi amesema watumishi wapya watakaokuwa wakiajiriwa wataanza kufanyiwa upekuzi wa kutosha kuhusu tabia na mienendo yao kulingana na majukumu na miiko ya taaluma zao ili kuwa na utumishi wenye taswira nzuri.
Aidha, Bw. Mkomi amewataka Waajiri kuimarisha mifumo madhubuti na taratibu za kuwalinda watoa taarifa juu ya vitendo vya ukiukwaji wa maadili na rushwa mahali pa kazi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news