Tanzania yazikutanisha nchi 20 mafunzo ya mifumo ya uangazi wa hali ya hewa duniani

DAR-Tanzania kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kwa kushirikiana na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) imekuwa Mwenyeji wa mkutano wa Mafunzo ya WMO kwa wataalamu wa hali ya hewa kutoka nchi wanachama wa WMO Kanda ya Afrika Mashariki na Kaskazini.
Lengo likiwa ni kuwajengea uwezo wataalamu wa Hali ya Hewa wanaofanya kazi katika vituo hivyo vya “WMO Regional WIGOS Centres (RWCs)” vya kanda ya Afrika Mashariki na Kaskazini Afrika.Akifungua rasmi mafunzo hayo yanayofanyika katika Hoteli ya Four Points by Sheratons, kuanzia leo Oktoba 7 hadi 11, 2024 mgeni rasmi na Mwenyekiti wa Bodi ya TMA, Mhe. Jaji Mshibe Ally Bakari amesema, suala muhimu kwa Taasisi za Hali ya Hewa za Afrika ni kuimarisha upatikanaji wa taarifa za hali ya hewa zenye ubora kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Pia, amesema mafunzo hayo yatasaidia kuboresha zaidi shughuli zinazofanywa, ikiwa ni pamoja na kuboresha mtandao wa kubadilishana data ili kuboresha zaidi utabiri wa matukio ya hali mbaya ya hewa katika nchi wanachama wa WMO.
Aidha, Jaji Mshibe ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuwekeza katika uboreshaji wa miundombinu ya huduma za hali ya hewa.

Jaji Mshibe amewashukuru pia WMO na washirika wengine kwa jitihada zao za kuimarisha huduma za hali ya hewa barani Afrika, ikiwemo kuanzisha mfuko wa uwezeshaji wa huduma za uangazi wa hali ya hewa.
Amesema, kupitia jitihada hizo, kiasi cha dola za kimarekani milioni 9 zimeidhinishwa kuboresha huduma za hali ya hewa nchini Tanzania.Awali, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Mwakilishi wa Kudumu wa WMO, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a ameeleza umuhimu wa kuimairsha uangazi na kuongeza upatakanaji wa data.
Ni kwa ajili ya kuimairsha utoaji wa tahadhari za matukio ya hali mbaya ya hewa na kukabiliana na changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa.

Aidha,Dkt. Chang’a ameeleza kuwa,Tanzania kupitia TMA imejipanga kuendelea kushiriki katika kuongoza na kuwa kinara katika baadhi ya jitihada za kuimarisha huduma za hali ya hewa barani Afrika.
"Tumejiandaa vyema kuwa mwenyeji wa Mkutano huu mkubwa wa Kikanda, na pia kama mwenyeji wa Kituo cha mfumo wa Kidunia wa kufuatilia vituo vya uangazi wa hali ya hewa kwa nchi za Afrika Mashariki,” amesema Dkt. Chang’a.
TMA itawasilisha mada zenye kueleza uzoefu wake katika utekelezaji wa jukumu hilo.

Kwa upande wake, Mwakilishi kutoka WMO,Abubakari Salih Babiker amesema, kumekuwa na changamoto ya matukio mbalimbali ya hali mbaya ya hewa hivyo ushirikiano wetu utasaidia katka kutoa tahadhari za mapema juu ya matukio ya Hali mbaya ya Hewa na tahadhali za mapema,”amesema.
Washiriki wa mkutano huo wametoka Taasisi za Hali ya Hewa za nchi za Tanzania, Tunisia, Algeria, Egypt, Sudan, South Sudan, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Somalia, Ethiopia, Djibouti, Madagascar, Comoros, Sychelles, Mauritius, Morocco, Afrika Kusini na waalikwa kutoka Oman na Sekretarieti ya Shirika la Hali ya Hewa Duniani.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news