Waziri Prof.Mkenda aipongeza BoT kwa kuelimisha umma masuala muhimu ya fedha

MBEYA-Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda, ameipongeza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa jitihada zake za kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala muhimu ya fedha, hususan utoaji wa leseni kwa taasisi ndogondogo za fedha, fursa za uwekezaji, na ununuzi wa dhahabu kutoka kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa dhahabu nchini.
Prof. Mkenda ametoa pongezi hizo alipotembelea banda la Benki Kuu wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho ya Nne ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa yanayofanyika katika uwanja wa Ruanda Nzovwe jijini Mbeya.
Kaimu Mkurugenzi wa Tawi la BoT Mbeya, Bi. Graceana Bemeye, akimkaribisha Waziri Mkenda kwenye banda hilo, alibainisha kuwa kumekuwa na mwitikio mkubwa kutoka kwa wananchi wanaotembelea banda la Benki Kuu.

Bi. Bemeye alisema kuwa wengi wamekua na shauku ya kujua jinsi Benki Kuu inavyopambana na ongezeko la taasisi zinazotoa mikopo bila leseni, kupitia mitandao na hata mitaani.
Mikopo hiyo isiyo rasmi, inayojulikana kama "mikopo kausha damu," imekuwa ikiathiri wananchi kwa kiwango kikubwa. 

Alieleza kwamba Benki Kuu inaendelea na jitihada za kutoa elimu ili kukabiliana na tatizo hilo katika jamii.

Aidha, Bi. Bemeye alisisitiza kuwa Benki Kuu itaendelea kuelimisha wananchi wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kuhusu umuhimu wa elimu ya fedha, ambayo ni msingi wa maendeleo ya uchumi wa nchi.
Maadhimisho hayo yenye kauli mbiu “Elimu ya Fedha, Msingi wa Maendeleo ya Kiuchumi” yanafanyika kuanzia tarehe 21 hadi 26 Oktoba 2024 ambapo yanahusisha taasisi mbalimbali za kifedha, ikiwa ni pamoja na mabenki, makampuni ya mitandao ya simu, mifuko ya pensheni, na taasisi za bima.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news