Zanzibar inaendelea kuchukua hatua kudhibiti maradhi ya kuambukiza kwa wanawake-Mama Mariam Mwinyi

ZANZIBAR-Mke wa Rais wa Zanzibar, Msarifu na Mwenyekiti wa Bodi ya wadhamini ya Taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF) Mhe. Mama Mariam Mwinyi amesema Zanzibar inaendelea kuchukua juhudi maaluum za kudhibiti maradhi ya kuambukiza yanayowapata kinamama kipindi cha ujauzito.Amesema, juhudi hizo zinalenga kuhakikisha ustawi wa mama na mtoto na udhibiti wa changamoto wanazokabiliana nazo, ikiwemo Ukimwi, kifua kikuu na utapiamlo.
Mama Mariam Mwinyi ameyasema hayo leo Oktoba 8, 2024 katika Hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa Ndege, Mkoa wa Mjini Magharibi alipofungua kongamano la siku tatu.Kongamano hilo linajadili masuala ya afya ya mama na mtoto hususani udhibiti wa maradhi TB, HIV na Malaria linalowashirikisha wataalamu wa Afya ya mama na mtoto kutoka Kenya, Nigeria, Tanzania na Skuli ya dawa za Kitropiki ya Uingereza.
Aidha, Mama Mariam Mwinyi amesema Zanzibar ni miongoni mwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara zenye idadi kubwa ya kinamama wanaojifungua, hivyo juhudi za pamoja za wadau na mashirika ya kimataifa zinahitajika kulipa kipaumbela suala la ustawi wa mama wajawazito na watoto.
Halikadhalika, amesisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya inashirikiana na Taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF) na kwamba wataendeleza programu tofauti ambazo tayari zimeanza kuleta mafanikio ya kunusuru maisha ya mama na mtoto ili kufikia malengo yaliyomo kwenye Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2025 na ile ya dunia ya 2030.
Mama Mariam Mwinyi ametoa wito kwa jamii, sekta binafsi na taasisi za kimataifa kuendeleza juhudi za pamoja kuhakikisha malengo hayo yanafanikiwa kwa kila mdau kutimiza wajibu wake kwenye eneo lake kwa dhamira ya kuwajengea mazingira bora kinamama wakati wa ujauzito, kujifungua na kuwa na uhakika maisha ya mtoto anayezaliwa.
Kongamano hilo la siku tatu litahitimishwa kwa kutolewa ripoti ya miaka mitano ya Mradi wa Udhibiti wa Afya ya mama na mtoto na kukinga na maradhi ya TB, Ukimwi na Malaria.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news